Dube aandika historia mpya CAF

WAKATI Yanga ikienda mapumziko ikiwa mbele kwa bao 1-0 dhidi ya Vital’O ya Burundi, mfungaji wa bao hilo la pekee hadi sasa, mshambuliaji Prince Dube, ameweka historia katika michuano hiyo akiwa nchini.

Yanga inacheza dhidi ya Vital’O katika mchezo wa mkondo wa kwanza wa raundi ya kwanza ya Ligi ya Mabingwa Afrika mchezo uliopigwa kwenye Uwanja wa Azam Complex, Chamazi jijini Dar es Salaam.

Dube amefunga bao dakika ya sita tu ya mchezo huo, lakini bao hilo limempa historia mpya akifunga la kwanza kwenye Ligi ya Mabingwa Afrika tangu atue Tanzania. Bao hilo lilitokana na pasi tamu ya kisigino ya Clatous Chama.

Dube amefunga bao hilo kwenye mchezo wake wa kwanza wa kimataifa wa mashindano akiwa mchezaji wa Yanga msimu huu akitokea Azam aliyoitumikia kwa miaka minne tangu atue nchini. 

Mchezaji huyo ambaye alitua Tanzania mara ya kwanza 2020 akiletwa na Azam hakuwahi kucheza Ligi ya Mabingwa ameandika historia hiyo akiwa na Yanga.

Mshambuliaji huyo raia wa Zimbabwe alifunga bao moja pekee kwenye mashindano ya Afrika akiwa na Azam akiifunga Bahir Dar Kenema kwenye Kombe la Shirikisho Afrika msimu uliopita, Azam ikilazimishwa sare ya mabao 2-2 kisha kutolewa kwa matuta 4-3 na Waethiopia hao.

AMKUMBUKA MKE WA TAJIRI
Wakati Dube akifunga bao hilo alionyesha fulana yake ya ndani iliyoandikwa maneno ya ‘Happy birthday boss of the boss’ akimtakia heri ya kuzaliwa mke wa mfadhili wa Yanga, Gharib Said Mohammed (GSM) ambaye jana alikuwa akikumbuka siku yake ya kuzaliwa.

Related Posts