Dar es Salaam. Tume Huru ya Taifa ya Uchaguzi (INEC) imetangaza nafasi za ajira za muda kwa ajili ya maandalizi ya Uchaguzi Mkuu wa baadaye mwaka huu, ikiwataka Watanzania wenye sifa kutuma maombi ya kazi ya usimamizi wa vituo vya kupigia kura.
Tangazo la nafasi za kazi zimetolewa Juni 28, 2025 na Mkurugenzi wa uchaguzi INEC, Ramadhani Kailima ikieleza mwisho wa kutuma maombi ni Julai 11,2025.
Taarifa ya tangazo hilo imetolewa kwa mujibu wa Kifungu cha 6(6) cha Sheria ya Uchaguzi wa Rais, Wabunge na Madiwani Na.1 ya mwaka 2024, kikisomwa pamoja na Kanuni ya 10(1) ya Kanuni za Uchaguzi za mwaka 2025.
Nafasi zilizotangazwa ni za wasimamizi wa vituo vya kupigia kura, wasimamizi wasaidizi na makarani waongozaji wapiga kura, ambazo zote ni kwa ajili ya kipindi cha uchaguzi.
Kwa mujibu wa INEC, waombaji wa nafasi hizo wanatakiwa kuwa raia wa Tanzania waliotimiza umri wa miaka 18 na si viongozi wa vyama vya siasa.
“Pia, wanapaswa kuwa na elimu ya kidato cha nne au zaidi, wawe na uwezo wa kusoma na kuandika kwa Kiswahili au Kiingereza, na wawe wakazi wa kata wanayoomba kufanya kazi. Aidha, waombaji wa nafasi ya karani wanapaswa kuwa waadilifu, watiifu na wenye akili timamu,”imeeleza taarifa hiyo.
Malipo kwa watendaji hao yameainishwa ambapo msimamizi wa kituo atalipwa Sh70,000 kwa siku kwa siku mbili, posho ya chakula ya Sh20,000 kwa siku moja na nauli ya Sh20,000.
Msimamizi msaidizi atalipwa Sh65,000 kwa siku (atalipwa ya siku mbili) pamoja na posho ya chakula na nauli sawa na msimamizi.
Kwa upande wa karani mwongozaji, atalipwa Sh65,000 kwa siku moja na posho ya chakula ya Sh20,000. Watendaji wote watakaoshiriki mafunzo watapewa posho ya Sh50,000 kwa siku na nauli ya Sh20,000 kwa kila siku ya mafunzo.
Tume imeeleza kuwa waombaji wote wanapaswa kuambatanisha nakala za vyeti vya sekondari na taaluma endapo wanavyo, wasifu (CV) unaoonesha anuani ya makazi, namba za simu, majina na namba za Nida za wadhamini wawili, pamoja na picha mbili za hivi karibuni za ukubwa wa pasipoti.
Pia, wanatakiwa kuwasilisha barua ya utambulisho kutoka kwa mtendaji wa serikali ya mtaa au kijiji wanakoishi. Watumishi wa umma wanatakiwa kupitisha maombi yao kwa waajiri wao.
Barua zote za maombi zinapaswa kuandikwa kwa anuani ya Mkurugenzi wa Uchaguzi, Tume Huru ya Taifa ya Uchaguzi, na kuwasilishwa kupitia kwa msimamizi msaidizi wa uchaguzi ngazi ya kata, ambaye atazifikisha kwa msimamizi wa uchaguzi wa jimbo husika.
Waombaji wanatakiwa kuandika nafasi wanayoomba nyuma ya bahasha ya maombi. Tume imesisitiza kuwa mtu yeyote atakayebainika kutoa taarifa za uongo au kughushi nyaraka atachukuliwa hatua kali za kisheria.