Waziri Kombo ashiriki Kongamano la Diplomasia ya Afya

Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Mhe. Mahmoud Thabit Kombo (Mb.) ameshiriki Kongamano kuhusu Kukuza Huduma za Afya Ulimwenguni kupitia Diplomasia lililoandaliwa na Chuo Kikuu cha Afya na Sayansi Shirikishi, Muhimbili (MUHAS) jijini Dar es Salaaam Julai 8, 2025.

Waziri Kombo ameeleza kuwa Sera ya Mambo ya Nje ya Mwaka 2001 toleo la mwaka 2024 iliyozinduliwa tarehe 19 Mei, 2025 na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan ilienda sambamba na uzinduzi wa Kitabu cha Mwongozo wa Diplomasia ya Uchumi kinachoeleza utekelezaji wa Diplomasia katika sekta mbalimbali ikiwemo ya afya.

Ameeleza kufurahishwa na wanafunzi wa MUHAS kwa kujipambanua mapema katika diplomasia ya afya kwani Tanzania sasa imekuwa kivutio kwa wengine kuja nchini kupata huduma mbalimbali za afya.

Hatua hii imesaidia kupunguza gharama ya kupeleka wagonjwa kutibiwa nje ya nchi. Hivyo, Kongamano hilo limelenga kuieleza Afrika na Dunia kuwa Muhimbili ipo tayari kuwahudumia kwa huduma bora na utaalamu wa hali ya juu.

Aidha, katika muendelezo wa kutekeleza Sera ya Mambo ya Nje kwa vitendo, Wizara pia ilishiriki mwaliko wa Mkuu wa Mkoa wa Dodoma kwenye kongamano lililofanyika mwezi Juni 2025, Dodoma kwa lengo la kutangaza fursa mbalimbali zilizopo mkoani humo ikiwemo huduma ya afya, elimu, biashara, uwekezaji na utalii kwa Mabalozi wote wanaowakilisha nchini.















Related Posts