ACT­-Wazalendo yataja mkakati kupunguza uharibifu wa mazao

Tunduru. Kuvuna tembo na kupitia upya mipaka ya hifadhi ni miongoni mwa mambo yatakayotekelezwa na Chama cha ACT –Wazalendo, ili kupunguza changamoto ya uharibifu wa mazao na madhara kwa binadamu inayosababishwa na wanyama hao.

Masuala hayo yatafanyika endapo ACT- Wazalendo itafanikiwa kushika dola katika Uchaguzi Mkuu wa Oktoba 2025 ambapo chama hicho kimewaomba Watanzania kuwaunga mkono katika mchakato huo.

Mambo hayo yameelezwa jana Jumatano Julai 9, 2025 na kiongozi mstaafu wa ACT -Wazalendo, Zitto Kabwe akiwahutubia wananchi wa Jimbo la Tunduru Kusini mkoani Ruvuma, katika mkutano wa hadhara uliofanyika Kijiji cha Namasakata wilayani Tunduru.

Mkutano huo wa hadhara ni sehemu ya ziara ya Zitto aliyeambatana na viongozi na wajumbe wa kamati kuu ya chama katika operesheni Majimaji Linda Kura, yenye lengo la kuwaamsha Watanzania kujitokeza kupiga kura na kuzilinda.

Viongozi wa ACT Wazalendo wakiwahutubia wananchi wa Jimbo la Tunduru Kusini mkoani Ruvuma katika mwendelezo ya ziara ya operesheni majimaji Oktoba Linda Kura



Kabla ya kueleza hayo, Zitto aliwaambia wananchi wa Tunduru Kusini kuwa jana alikuwa Namtumbo ambapo alipokea kilio cha tembo kutoka kwa wananchi wa wilaya hiyo.

“Nilikuwa nasoma gazeti la Mwananchi la Desemba 12,2024 na mwandishi anaitwa Kalunde Jamal aliyeandika makala kuhusu namna ambavyo tembo wanavyoharibu mazao na kuleta madhara kwa wananchi katika mikoa ya Kilimanjaro na Singida,” amesema Zitto.

Ripoti maalumu iliyofanywa na Mwananchi mwaka 2024 ilibainia athari kubwa zinazotokana na wanyama hao, katika mikoa ya Singida na Kilimanjaro. Pia ilibaini tembo si kuharibu mazao pekee, bali pia wanasababisha vifo na majeraha kwa wakazi wa maeneo hayo.

Kutokana na hilo, Zitto amesema ACT- Wazalendo ikishinda uchaguzi mkuu itaweka utaratibu wa kuwavuna tembo ili kuwapunguza, akisema njia hiyo ni sayansi inayoelekeza hivyo kila baada ya muda ili kuwapunguza.

“Wakipungua, watapunguza uharibifu wa mazao na madhara kwa binadamu. Jambo jingine tutakalolifanya lazima tupitie upya mipaka ili kuwapa wananchi maeneo makubwa zaidi ya kufanya shughuli zao za kiuchumi na kuweka hifadhi mbali.

“Tutahakikisha kunakuwa na uvunaji wa tembo, sasa hivi kila maeneo tembo, tembo…lakini kubwa kuliko zote ni kuiondoa CCM katika uchaguzi mkuu wa Oktoba,” amesema Zitto ambaye ni mbunge wa zamani wa Kigoma Mjini.

Awali, Katibu wa ACT- Wazalendo mkoa wa kichama Selous, Mtutura Abdallah ambaye ni mtia nia ya ubunge wa Jimbo la Tunduru Kusini amesema kumekuwa na changamoto ya tembo katika Wilaya ya Tunduru na kusababisha uharibifu wa mazao.

Mbali na hilo, Mtutura aliyewahi kuwa mbunge Tundura kwa tiketi ya CCM, amewaomba wananchi wa wilaya hiyo kukichagua chama hicho katika uchaguzi mkuu wa Oktoba ili wakakatue changamoto za uharibifu wa mazao ya wananchi.

Mjumbe wa Kamati Kuu ya ACT- Wazalendo, Halima Nabalang’anya amesema wananchi wa Tunduru wamekuwa washiriki wazuri katika chaguzi mbalimbali lakini changamoto inakuwa katika umaliziaji.

Viongozi wa ACT Wazalendo wakiwahutubia wananchi wa Jimbo la Tunduru Kusini mkoani Ruvuma katika mwendelezo ya ziara ya operesheni majimaji Oktoba Linda Kura



“Tatizo ni umaliziaji tu, lakini safari hii, ACT- Wazalendo tumejipanga ipasavyo na tutahakikisha anayeshinda anatangazwa,” amesema Nabalang’anya ambaye ni waziri kivuli wa uchukuzi katika chama hicho.

Related Posts