Na Bakari Madjeshi, Michuzi TV
Rais wa Heshima na Mwekezaji wa Simba SC, Mohammed Dewji (Mo Dewji) amethibitisha kuwa kutoka mwaka 2017 hadi mwaka 2024 ametumia zaidi ya Shilingi Bilioni 80 (Tsh. 87 B) kwenye masuala mbalimbali kwa ajili ya Klabu hiyo.
Mohammed amesema hayo kupitia ‘video’ yake aliyoichapisha kwenye mtandao wa ‘Instagram’. Amesema kiasi hicho cha pesa ametumia Shilingi Bilioni 45 kwenye kulipa mishahara,usajili, maandalizi na masuala mengine ya uendeshaji wa timu.
Mo Dewji amesema kiasi cha Shilingi Bilioni 20 amekitoa kama sehemu ya ununuzi wa hisa (49%) ndani ya Simba SC. Pia, amesema mara nyingi ametoa msaada nje ya mfumo rasmi kila palipohitajika uhitaji wa dharura.
Kupitia taarifa hiyo, Mo Dewji amesema kuwa dhamira yake ni kuiona Simba SC inatwaa ubingwa wa Afrika, hivyo amewaomba wanachama na mashabiki kuwa kitu kimoja ili kutimiza malengo.