Baada ya kuchoka msongamano wa Bongo isiyo na bongo za kutatua changamoto na kero zake, nimechemsha bongo. Niwajuze waziwazi. Nina mpango wa kununua na kufunga king’ora kwenye mchuma wangu kuepuka kusota kwenye foleni kama mafyatu makapuku wakati mie ni munene wao kama wale wanene wa kaya.
Maana, kama sikosei, ndiyo mfumo wa kifyatu wa wanene kuwafyatua wachovu waliofyata badala ya kufyatuka na kufyatua wale wanaowafyatua tena kifalafala kama hivi. Kifyatu, hii inaitwa sera ya kujipendelea au kujihudumia ukijidai unawahudumia. Unawahujumu badala ya kuwahudumia kwa vile hawawezi kujihudumia kwa kukufyatua.
Unaweka ving’ora kwenye ndinga za wanene hata wale uchwara hukwepa madhara kiasi cha kutotafuta suluhu ya tatizo la msongamano. Zamani, wanene wakila baada ya wanyonge kula. Siku hizi, ni tofauti. Wanene wanafyatua kila kitu wakati wote tena bila aibu.
Hakuna cha wanyonge wala wanyongwaji. Hizi zama za wanyongaji kuwanyonga wanyongwaji. Na hii, kinene, inaitwa haki ambayo hutokana na amani, utulivu, na “mshikamano” hata kama ni vya imani. Huoni kinavyoshikana barabarani siku hizi?
Kwa vile hakuna kisichowezekana kwa mafyatu, wakiamua, nami lazima nifyatue king’ora kuepuka msongamano usababishwao na ukosefu wa ubunifu na uzwazwa wa kimfumo na kijamii.
Kwanza, inakuwajekuwaje jamii nzima inaparaganyikiwa na kukosa mfumo uingiao akilini? Kwa vile mie mjanja tena mwenye akili kubwa ambaye nimeamua kuzitumia kuweka king’ora, hili swali si langu bali lako.
Pili, kwa vile mimi ni munene wa mafyatu tena mjanja wa aina yake, na familia na washikaji wangu lazima waufaidi unene wangu. Hivyo, napanga kufyatua ving’ora kama sina akili nzuri. Nahakikisha, kama ndata na wanene wengine, bi Mkubwa wangu na kitegemezi chetu nao wanakuwa na ving’ora kwenye ndinga zao.
Bila kufanya hivyo, bi Mkubwa anaweza kuwa anachelewa kila aendapo kusuka au kuchonga na mashoga zake huku kitegemezi kikichelewa shule. Sipati picha vitegemezi visivyo na ving’ora vinawezaje kuwahi shule na kusoma kama itakiwavyo mbali na kuamsha mapema na kuchelewa kurejea nyumbani.
Tatu, licha ya kuweka ving’ora kwenye ndinga zetu, nataka kuanzisha utaratibu wa kufunga barabara ili misafara yetu ipite hata kama tunakwenda kupiga ulabu.
Who cares kama mafyatu wameshindwa kufyatuka na kufyatua hadi wakafyata na kufyatuliwa kirahisi hivi unataka nifanye nini zaidi ya kuwafyatua kama wale wanaowafyatua nao wakafyata?
Nne, rasmi kuanzia sasa, nitahakikisha kila bodaboda itakaribia nilipo au kunipita, kufunga njia, au kujishebedua na kujifanya ina haraka, nachukua cha moto mkononi ili wakigonga ndinga yangu niwawahi kabla hawajaniwahi. Bila cha moto usawa huu, sijui nani atakuwa salama.
Tano, kuanzia sasa, nataka kununua magwanda kama ya ndata ili ikitokea kikaumana au kunuka, mafyatu wajue mie ni ndata. Hivyo, wanigwaye hata kama nitagonga mikweche na ngwalangwala zao uchwara au siyo? Maana, usawa huu, bila kwenda kindavandava mambo hayaendi zaidi ya kuishia kufyatuliwa hivi hivi ukijiona kama kaya ilivyofyatuliwa hadi wenye akili kuhoji utimamu wa akili zetu.
Sita, baada ya kufunga king’ora, sitapita kwenye barabara za kawaida zilizojaa mikweche na misongamano. Yangu ni Mwendo Kasi tena kwa kasi na visasi kama wenye ving’ora na bodaboda wafanyavyo bila kustukiwa wala kupewa adhabu japo ya faini. Unacheza na kaya hii isiyo na mpangilio wala mfumo vinavyoelekea zaidi ya vurugu? Kila fyatu anatungia na kujichagulia sheria yake.
Taa ikizuia, bodaboda anakula mwendo. Ikiruhusu kwenda kulia, yeye anakwenda kushoto tena na ndata wanaangalia. Sijui wapo pale kama au maua au mapambo au kuna jambo? Mbona nasikia kwa Ka-game wanafuata sheria kama madereva wengine?
Kwani, hapa tatizo ni bodaboda au wanene walioruhusu hii vurugu. Au nishauri mafyatu watumie bodaboda tuone itakuwaje. Kama mbwai mbwai du. Ama kweli kaya imefunguka kiasi cha barabara kufungwa kwa mafanikio. Hapa lazima tuseme wazi. Bodaboda mnaupiga mwingi.
Saba, kwa vile mimi ni munene na nina mtandao mkali, napanga kupeleka kitegemezi chetu kusome majuu kuepuka kuzeekea kwenye ngwalangwala kikienda shule ambako bila shaka kitafeli tu. Unacheza na foleni na vurugu siyo?
Nane, napanga kuitisha bunge la mafyatu ili kutunga sheria mpya ambayo itaitwa uhasama na vurugu barabarani badala ya ile ya usalama barabarani ambayo imegeuka fujo barabarani. Hapa, nitapendekeza taa na vitochi na matrafiki wote waondolewe barabarani ili kupunguza fujo na vurugu. Nitashauri hata mataa ya barabarani yaondolewe na kuweka tunguli. Maana, Waswahili wanavyoogopa tunguli, bila shaka, watazitii kinyume na wanavyodharau mambo ya sayansi na tekelinalokujia.
Mwisho, kwa vile ving’ora vinalipa na kuepusha usumbufu na vurugu, napendekeza wajanja wote tuwe navyo ili kuepuka kunyotolewa roho na misongamano na misongo ya mawazo vitokanavyo na uholela huu na uzwazwa vya kujitakia. Ving’ora hoyeee! Du! Kumbe naota mchana!