Ukijua thamani na majukumu unayotakiwa kutimiza katika maendeleo na maisha ya watoto wako, hilo litakusaidia kujitoa kikamilifu na kuwekeza katika familia.
Kinababa wengi wanaamini kwamba wao jukumu lao ni kutunza familia na sio kulea watoto wao.
Mwanaume anayejiona kuwa “hana uwezo” hayuko kwenye nafasi nzuri ya kusaidia, kulinda, kuongoza na kuandaa wakati ujao mzuri kwa watoto na familia yake kwa ujumla. Kuna mambo saba yanayopendekezwa ambayo yanaweza kukusaidia kuwa baba bora. Mambo haya ni kuwa na uhusiano mzuri na mama wa watoto; kutumia wakati pamoja na watoto wako; kutunza watoto; kusimamia nidhamu watoto kwa njia inayofaa.
Mengine ni kuwa kiongozi wa kuwaelewesha watoto kuhusu ulimwengu; kuwalinda na kuwaandalia mahitaji yao na kuwa mfano mzuri kwa watoto wako.
Huenda baba asiweze kufanya mambo yote saba kwa ukamilifu, lakini baba anayejitahidi kufanya vizuri kati ya mambo hayo, atawasaidia watoto na familia nzima kwa ujumla. Hapa ninayaeleza majukumu haya kwa kina.
Kuwa na uhusiano mzuri na mama wa watoto: Moja kati ya njia muhimu za kuwa baba bora ni kumtendea mama wa watoto wako kwa upendo, heshima, na kumfikiria (iwe watoto wameoa au wataoa baadaye).
Mfano ambao baba anaweka kwa kuwa na uhusiano mzuri na mama yao, unaandaa kielelezo kizuri kwa watoto. Watoto ambao wanamwona baba akimtendea mama yao kwa upendo, heshima na kujitoa kwa ajili yake, inaelekea kwamba wao pia wataiga mfano wake kwa kuwatendea kwa njia hiyohiyo, rafiki, wachumba au wake zao.
Tumia wakati pamoja na watoto: Jambo muhimu kwa watoto ni muda unaotumia pamoja nao.” Alisema Dk Ken Canfield, ambaye ni mwanzilishi wa taasisi ya President, National Center for Fathering.
Muda ambao baba anatumia na watoto wake ni muhimu kwa sababu tatu. Kwanza, kutumia wakati pamoja na watoto kunamwezesha baba kuwajua vizuri watoto na wao kumjua baba yao.
Baba anaweza kugundua tabia nzuri na mbaya, matumaini na hofu, mawazo na mambo wanayopenda kwa kutumia wakati pamoja na watoto wake.
Pili, baba anayetumia muda mwingi pamoja na watoto anakuwa na uwezo mkubwa wa kuwatunza na kuwajali. Muda ambao baba anatumia pamoja na watoto wake, unamwezesha kutambua mahitaji muhimu ya watoto kama vile uhitaji wa kupendwa, uangalifu, mwongozo na nidhamu.
Tatu, kama inavyoonyeshwa katika nukuu hapo juu, mara nyingi watoto wanaona kuwa kutumia wakati pamoja nao, ni njia bora inayoonyesha kuwa mzazi anawapenda.
Watunze watoto wako: Matunzo ya baba hutimiza makusudi mbalimbali muhimu kama vile kumsaidia baba kuwa na uhusiano mzuri na watoto wake; kuchochea hali nzuri ya kisaikolojia na kujielewa kwa watoto.
Pia kuandaa mfano mzuri wa kuigwa na watoto, kuwalinda watoto wa kike kujiingiza katika uhusiano wa mapema ili kukidhi haja ya kupendwa na mwanaume.
Tangu wakiwa wachanga baba anapaswa kuwajibika watoto wanapolia, awashike, kuwakumbatia mara kwa mara, na kushiriki kwa njia mbalimbali kuwatunza.
Katika maisha yote ya utoto, baba anapaswa kuwa mstari wa mbele kuwapongeza watoto wake wanapokuwa na tabia nzuri au wanapotimiza jambo, wakumbatie na kuwabusu mara nyingi, wafariji wanapokuwa na huzuni au woga.
Baba anapaswa kuwapongeza vijana wake hasa pale wanapotimiza jambo kubwa au muhimu. Utunzaji wa baba huenda usionekane sana kama ule wa mama.
Kwa kweli, njia moja ya msingi ambayo baba anaweza kuitumia kuwatunza watoto wake hasa wale wachanga na vijana ni kwa kutokasirika wakati mtoto anasumbua au kucheza.
Simamia nidhamu ya watoto kwa njia inayofaa: Baba anawezaje kuwapa nidhamu watoto wake? Kwanza kabisa, baba anahitaji kudhibiti hisia na matendo yake anapowatia nidhamu watoto wake.
Kinababa wanaowafokea watoto wao au kuwapiga vibaya wanashindwa kuwatia nidhamu watoto wao kwa njia nzuri, kwa sababu mbili, wanawawekea wao mfano mbaya na pili kwa sababu wanapoteza heshima yao kwa watoto wanaposhindwa kudhibiti hisia na kuacha hisia ziwaongoze. Kwa kusikitisha, kinababa wengi wamekuwa na tabia hizi kwa sababu ya kuchanganyikiwa wanapohisi kwamba hawana uwezo wa kuwaongoza watoto wao. Hilo hutokea kwa sababu hawadhibiti hasira zao, au kwa sababu hawajui njia nyingine ya kufanya.