Mamlaka ya Usimamizi wa Wanyamapori Tanzania (TAWA), kupitia Kanda ya Kaskazini, inaendelea kutumia jukwaa la Maonesho ya Nane Nane 2025 yanayoendelea katika Viwanja vya Nane Nane mkoani Arusha kuwafikia Watanzania kwa kuwapatia elimu kuhusu uhifadhi, utalii na fursa za uwekezaji katika maeneo yake ya usimamizi.
Kupitia ushiriki wake ndani ya banda la pamoja la Wizara ya Maliasili na Utalii, TAWA inatoa taarifa na elimu kwa umma kuhusu vivutio vya utalii vilivyoko Kanda ya Kaskazini na maeneo mengine nchini, sambamba na fursa za uwekezaji katika sekta ya uhifadhi. Maonesho hayo yaliyoanza rasmi tarehe 1 Agosti 2025 yamekuwa jukwaa muhimu la kuwasiliana moja kwa moja na wananchi.
Mbali na utoaji wa elimu, TAWA kwa kushirikiana na wadau wake imewavutia wananchi kwa kuonesha Wanyamapori hai wakiwemo Simba, Fisi na Mamba ambao wamekuwa kivutio kikubwa kwa wageni mbalimbali kutoka ndani na nje ya Mkoa wa Arusha wanaotembelea banda la Maliasili na Utalii.
Takwimu za awali zinaonesha kuwa kufikia tarehe 3 Agosti 2025, zaidi ya wananchi 350 wamepokea huduma ya elimu na maelezo kutoka kwa wataalamu wa TAWA. Kazi ya uelimishaji na uhamasishaji inaendelea hadi kilele cha maonesho hayo mnamo tarehe 8 Agosti 2025.
