Uwekezaji wa Serikali ulivyopaisha mapato Rungwe

Mbeya. Kufuatia Wakulima Wilaya ya Rungwe Mkoa  wa Mbeya  kuchangamkia fursa ya matumizi ya   mbegu bora ya viazi mviringo maarufu  kama ‘Obama’, Halmashauri hiyo  imefanikiwa kukusanya mapato ya ndani ya zaidi ya  Sh1.5 bilioni kwa mwaka.

Hatua hiyo imetajwa kufanikisha kuongeza  uzalishaji kutoka wastani wa tani  513,313, hadi  tani 614,278 kwa kipindi cha mwaka 2021/2025 .

 Ofisa Kilimo Halmashauri  ya Rungwe,  Majaliwa Mwalembe ameliambia  Mwananchi  Digital leo Agosti  6,2025 kwenye banda la Maonyesho  ya  Wakulima Nanenane katika Viwanja vya John Mwakangale mkoani hapa.

Maonyesho hayo yanahusisha taasisi mbalimbali za Serikali na wadau wa sekta ya kilimo kutoka mikoa ya Nyanda za Juu Kusini hususani Njombe, Iringa, Rukwa, Katavi, Songwe na Mkoa mwenyeji wa Mbeya.

Amesema Wilaya  ya Rungwe  wananchi wengi wamegeukia  shughuli za kilimo cha  mazao ya chakula na biashara kama ndizi, parachichi, huku viazi mviringo vikipewa kipaumbele.

“Asilimia 75 ya mapato ya halmashauri hutokana na kilimo,lakini tutokana na mchango mkubwa   tumeweka mazingira  mazuri ya kuwasajili  kwenye vikundi na kupewa elimu ya kilimo bora, upimaji wa afya ya udongo  sambamba na upatikanaji  wa mbolea za ruzuku na mikopo asilimia 10,”amesema.

Katika hatua nyingine amesema ili kufikia malengo ni Serikali ya kuongeza  tija kuzalisha  mazao ya kimkakati wamejipanga kukabiliana na changamoto   za masoko kwa kudhibiti madalali na vifungashio vya mifuko la lumbesa.

Ametaja moja ya sifa iliyo wasukuma wakulima  kutumia mbegu  bora ya viazi mviringo  aina ya Obama ni kutokana na kufanya vizuri  katika uzalishaji ambapo kwa hekari moja wanavuna gunia  80 mpaka 100.

“Kiazi Obama kinafanya vizuri sana katika uzalishaji  endapo mkulima akazingatia kanuni bora kuweka mbolea kwa wakati na kupima afya ya udongo kabla ya kuanza uzalishaji, lakini pia kinafanya vizuri sokoni,” amesema.

Amesema ili kuimarisha  masoko na kuongeza  tija ya uzalishaji  wameweka mikakati kuhakikisha wakulima wanapata  mikopo asilimia 10 kwa kuzingatia  kilimo kinahitaji mtaji.

Mwalembe amesema wana wahimiza  maofisa kilimo kuwafikia wakulima kutoa elimu ya uzalishaji ulio na tija kwa kuzingatia  mabadiliko ya tabianchi ili kufikia malengo ya Serikali kuwa na ziada ya chakula.

Amesema kwa msimu wa  mwaka jana bei ya  viazi mviringo ilikuwa juu kwa  Sh 37,000 mpaka Sh50,000 kwa ujazo wa kilo 100 hadi 105 ,lakini msimu huu  imeporomoka hadi kufikia Sh25,000 mpaka Sh30,000.

Ametaja sababu ya kuporomoka kwa soko ni kutokana na kujiendesha lenyewe hususani  kuingiliwa na wimbi la madalali wanaotumia vifungashio  vya mfumo  wa lumbesa  ambayo  imepigwa marufuku na Serikali.

Kwa upande wake Ofisa Biashara Wilaya ya Rungwe, Renatus  Nicolaus  amesema masoko ya mazao yanayozalishwa masoko yake makubwa yako Jijini Dar es Salaam, Mwanza na Dodoma na mikoa mingine inachukua, lakini sio kwa kiwango kikubwa.

“Ardhi ya Rungwe ni nzuri hata ukiangalia mazao yak e hususani viazi ingawa kuna shughuli za ufugaji wa ng’ombe wa maziwa ambayo pia yana masoko hususani  kuanzishwa kwa viwanda vidogo vya kuchakata na kuongeza thamani,”amesema.

Naye Mkulima wa viazi katika Kata ya Simambwe Wilaya ya Mbeya, Sikujua Joram amesema kilio  hao kikubwa ni madalali na ununuzi wa mifuko la kumbesa ambayo inawanyonya.

“Miaka nenda miaka rudi kilio  chetu ni madalali  na kumbesa tunaona jitihada za serikali, lakini kundi hilo ni kubwa tunaomba tutafutiwe soko la uhakika ili tuweze kunufaika na kilimo kwani tunatumia nguvu kubwa kuzalisha  wengine wananufaika,”amesema.