Dar es Salaam. Magonjwa ya shambulio la moyo (heart attack) huwaathiri zaidi wanawake kuliko wanaume, huku ikielezwa kuwa Watanzania wanakimbilia zaidi India kutibiwa magonjwa ya mifupa.
Hayo yameelezwa na Daktari Bingwa wa Magonjwa ya ndani ya mwili Narendra Swamy, kutoka Hospitali ya Ramaiah ya India alipokuwa katika mahojiano maalumu yaliyofanyika leo Jumatano, Agosti 6, 2025.
“Tumebaini kuwa wanawake wanaathiriwa zaidi na magonjwa ya moyo kuliko wanaume na ndiyo maana ni muhimu kuelimisha ili kujua dalili na namna ya kudhibiti magonjwa hayo,” amesema Dk Swamy.
Dk Swamy ambaye pia ni Mkurugenzi Mtendaji wa Ramaiah Hospitali ya India amesema sababu za magonjwa ya shambulio la moyo kuathiri zaidi wanawake kuliko wanaume ni wanawake kutokufanya mazoezi na vichocheo (hormones) alivyo navyo mwanamke.
“Magonjwa huwaathiri wanawake kwa namna yao, kulingana na maumbile na mtindo wao wa maisha,” amesema Dk Swamy.
“Wanawake walio wengi wanaogopa kuzungumza wazi kuhusu magonjwa yanayowathiri; Wanamke huathiriwa kwa namna tofauti kulingana na umri, uzazi, ndoa, na balehe,” amesema Dk Swamy.
Siri kupambana na saratani
Akifafanua kuhusiana na ugonjwa wa saratani, Dk Swamy amesema hakuna sababu maalumu iliyothibitishwa kuwa ndicho chanzo cha saratani duniani.
Hata hivyo amesema, kuna njia za kuzuia uwezekano wa kupata saratani na kusema, kufanya mazoezi yakiwamo ya kutembea kwa angalau dakika 30 kwa siku.
“Jambo la pili ni kuishi maisha ya afya, usile sana wala usile kidogo kupita kiasi, kisha ni muhimu kufanya uchunguzi wa afya kila uwezapo,” amesema.
Pamoja na kutoa ushauri wa kiafya, Hospitali ya Ramaiah imeipongeza TAMWA (Chama cha Wanahabari Wanawake Tanzania) kwa kuinua na kuwezesha wanawake, na hivyo imetoa nafasi ya mafunzo kwa wanachama chama hicho.
“Tutashirikiana kutoa mafunzo kwa wanachama wa Tamwa, madaktari wetu watatoa mada kadhaa zinazowahusu wanawake ikiwamo ukomo wa hedhi, balehe na magonjwa mengine yasiyoambukiza,” amesema.
Amesema Dk Swamy amesisitiza kuwa magonjwa mengi yanatokana na sababu kuu mbili ambazo ni vinasaba (genetics) pamoja na mitindo ya maisha, hivyo ustawi wa afya ya jamii yeyote ile unategemea mitindo bora ya maisha ambayo itasaidia jamii yetu.
Pamoja na kutoa ushauri wa kiafya, Hospitali ya Ramaiah imeipongeza Tamwa kwa kuinua na kuwezesha wanawake,kutoa elimu ya haki za wanawake wasichana na watoto ikiwemo afya na hivyo imetoa nafasi ya mafunzo kwa wanachama chama hicho.
Kadhalika Dk Swamy Ramaiah imesisitiza kuwa Hospitali ya Ramaiah itatoa matibabu kwa mgonjwa mwenye uhitaji ambae Tamwa itamtambulisha kwao ili kurudisha hisani kwa jamii kwa kile inachofanya.
“Mnafanya kazi bora sana kwa wanawake hivyo kwa usimamizi wenu, iwapo kutakuwa na mgonjwa mwenye uhitaji, sisi tutashiriki kumsaidia matibabu,” amesema.
Mkurugenzi wa Tamwa, Dk Rose Reuben amewashukuru Ramaiah kwa ushirikiano ambao wamekuwa wakiutoa katika shirika lao ikiwemo elimu ya magonjwa mbalimbali ambayo yanawasumbua wanawake wa umri tofauti.
“Ushirikiano huu ni muhimu kwani jamii yetu inahitaji kuelewa mambo mengi yatakayowawezesha kujikinga na magonjwa kwani kinga ni bora kuliko tiba,” amesema.
Mitindo ya maisha ya watu waishio mjini mara nyingi inawakwamisha kufanya mazoezi na kula chakula chenye virutubisho vya kutosha kwa wakati hali inayosababisha ongezeko la magonjwa yasiyoambukiza kama vile shambulio la moyo.
Katika mahojiano hayo, Dk Swamy amesema, hospitali ya Ramaiah, inapokea zaidi wagonjwa wa mifupa, ikiwamo uchakavu wa mifupa, uti wa mgongo, mifupa kuwa dhaifu, mgongo kujikunja na mvunjiko wa mfupa.
“Pamoja na hayo wagonjwa wa saratani pia wanapokewa kwa wingi hapa kutoka Tanzania na tunawahakikishia kuwa huduma zetu ni rafiki na hospitali hii si ya kujiendesha kwa faida ni kwa ajili ya kuhudumia zaidi,” amesema.