Dar-si-Salama ilivyomfyatua Fyatu na yeye akafyatuka!

Baada ya kukaa majuu kwa ngwe nyingi, kfyatufyatu si nikajitia kiherehere na mbambamba kwenda kujinoma Dar––si––Salama.

Badaa ya kwenda Arusha, Moshi, na Ushoto na kufaidi kila kitu na makandokando, likaja wazo la kufyatua kitu hiki na namna nilivyofyatuliwa kulhali.

Bila hili wala lile, niliamua kutua Dar-si-Salama japo kujikumbusha zama zangu Dar. Mara hii, sikufikia Kariakoo nilipokulia. Badala yake, nilijinoma Mikocheni kwa Warioba tulipopiga kambi kabla ya kukitoa na kuelekea South.

Nigefikiaje sehemu ambayo imeharibiwa na kuharibika kiasi cha kutorekebishika? Kabla ya hapo, tulifikiria kutua KIA ili tujinome zetu Arushwa, sorry, Arusha tukidhani bado inazo sifa na ujiko wake vya zama zile za dhahabu ilipokuwa Dar Salaama na si Dar-si-Salama au Dar-al-shari yenye fujo na misongamano. Bwana mdogo Sirili analijua hili vizuri.

Kwa uamuzi huu, wacha yanikute ya kunikuta kiasi cha kuapa na kujuta kuwa sitafanya kosa hili tena vinginevyo mambo yabadilike kama yatabadilika au mafyatu wafyatuke na kuyaweka sawa badala ya kuwekwa sawa na wale wanaowaweka sawa aka kuwafyatua wakidhani wako sawa wakati si sawa.

Hata hivyo, ni miujiza gani itatokea mambo yabadilike wakati wahusika wamegoma kubadilika? Nani atabadilisha nini wakati wanaopaswa kubadilika wamebadilika kwa kutobadilika? Ile kutia guu kwenye uwanja wa mapipa wa Mwalimu Mchonga nilishangaa sana namna jiji lilivyobadilika hata kuharibika, niseme kuharibwa kwa sababu hadi sasa, sijazijua hasa nikikumbuka namna Mwendaze Joni Kanywaji Makufuli alivyokuwa ameupendelea akitaka uwe kama majuu. Nilifurahia mijengo inayoota kama uyoga tena haraka bin vuu.

Sambamba, nilijikuta nikishuku, kuhuzunika, na kulaumu kwa sababu ya kutojua kama ujenzi au tuseme uoteshaji wa mijengo hii unafuata sheria na taratibu ili baadaye isigeuke makaburi ya halaiki itakapoanza kuporomoka kama maadili yaliyosababishwa na kupanda kwa madili ambayo ni chanzo kikubwa cha yote haya.

Hakika, nilifurahia ongezeko la ndinga japo nilisikitishwa na namna zinavyotumika hovyo mbali na kusababisha mateso, misongamano, uchafuzi wa mazingira na usumbufu usiomithalika.

Pia, nilihuzunika kushuhudia namna mafyatu wanajipa moyo kuwa mambo yatakuwa poa soon.  How soon is soon? Nani atayafanya yawe poa wakati wanaopaswa kufyatuka na kufyatua wanaowafyatua wamepoa kama siyo kupozeshwa na wale wanaowafyatua tena kijingajinga? Baada ya kutua home na kupumzika si nikaamua kwenda kuwatembelea maswahiba zangu wa mitaa ya Msimbazi na Mbaruku na kuhami msiba wa ndugu rafiki na fyatu Hussein Ahmed (RIP).

Wee, nani angeamini kuwa ingenigharimu wiki nzima njiani kuendesha sehemu ambayo zama zile za dhahabu ilitumia dakika kumi!

Kwanza, sikuamini kuwa kuna fyatu mwenye akili zake, hata ziwe mbaya au pungufu vipi angeweza kuendesha chombo cha moto kuelekea upande usioruhusiwa au kukatisha kwenye taa nyekundu wakati akijua madhara ya kufanya hivyo kwake na wengine. Kitu kingine, mafyatu wa Dar wanaishi kila fyatu kivyake kana kwamba wanaishi peke yao. Hakuna anayejali hatari au uwepo wa wengine.

Kila fyatu anataka awahi bila kujua kuwa anaweza kuwahi au kuwawahisha wenzake kaburini au mochwari! Pili, hadi sasa sijajua kama Dar si Salama ina wabobezi wa upangaji miji mbali na wenye akili lau timamu kuona haya yanayofanyika kiasi cha kuathiri uchumi wa jiji na mafyatu binafsi kutokana na kupoteza muda kwenye misururu mbali na kuongeza carbon print bila sababu.

Je, wachumi siyo wachumia tumbo, wanasemaje kuhusiana na kufyatuliwa huku kwa mafyatu na Dar yao?

Tatu, siamini kuwa kuna mafyatu wenye akili wasioona hatari inayosababishwa na uendeshaji vyombo vya fire bila kufuata kanuni na sheria. Nne, hadi sasa siamini kuwa kuna mafyatu wanene wenye akili wanaoona ninayoona halafu wakayafumbia macho na kutafuta majibu ambayo kimsingi, si majibu bali matatizo zaidi kama kujipendelea kwa kutumia ving’ora.

Ili kuondoa misongamano na uchelewaji na upotevu wa fedha na muda, napendekeza kila fyatu awe na king’ora hata kwenye baiskeli ili asichelewe aendako. Sijui hapa nani anamdanganya au kumfyatua nani wakati wote ni wahanga wa jinai hii ya kujitakia kutokana na tamaa, ubinafsi, na uzwazwa?

Tano, nilishangaa kuona mafyatu wakifanyia biashara mashimoni pale Karia koo. Sehemu wanazofanyia hasara, sorry, bihasara ni hatarishi kwao na wateja wao.

Kuna joto la kuua fyatu mbali na mikelele ya matangazo ya biashara uchwara pale maeneo ya Karumekenge. Ukikaa pale muda mrefu, kama hugeuki kichaa ujue ulishakuwa kichaa tayari au una changamoto ya afya ya akili ambayo huijui wala kujijua.

Kimsingi, mafyatu wote unaowaona pale wakiuza au kununua wana changamoto hii au kwa lugha ya kitaalamu ni vichahaa.

Nini kiliikuta Dar yetu kiasi cha kugeuka kero badala ya Bandari Salama iliyogeuka Bandari Shari? Je, nini kifanyike kuinusuru Dar yetu tuliyoipenda na kuizoea? Je, hakuna namna ya kufanya hivyo? Kwanini wengine waweze sisi tushindwe?

Hayo ndiyo mafyatuzi na masahibu yaliyonikuta na ujumbe wangu Dar kabla ya kukitoa kuelekea J’burg South. Kumbe nimeishafika Ukanadani!