Askofu Mapunda asisitiza haki kuelekea uchaguzi mkuu

Mbeya. Askofu wa Kanisa Katoliki Jimbo la Singida, Edward Mapunda amewatahadharisha Watanzania kutorubuniwa kwa rushwa na kuomba haki itendeke kwenye uchaguzi mkuu Oktoba 29 mwaka huu wa kuchagua  Rais, Wabunge na Madiwani na kusisitiza atakayeshinda ashinde kwa haki.

Hatua hiyo imetajwa ni kuhepusha  migogoro sambamba na kusisitiza  watakao shindwa wakubali  matokeo  ili kulinda amani ya nchi.

Mapunda ambaye  pia ni Mwenyekiti  wa Idara ya Utume wa Walei  Baraza la Maaskofu Tanzania (Tec), ametoa angalizo hilo leo Jumamosi ,Agosti  23,2025 wakati wa ibada maalum ya kuliombea taifa katika  kuelekea uchaguzi  mkuu Oktoba mwaka huu.

Ibada hiyo ilianza kwa maandamano na kuelekea Chuo Kikuu cha Kikatoliki  (CUoM), sambamba na kuhitimisha Kongamano  la sita kitaifa la Vijana Wakatoliki Wafanyakazi   (Viwawa), lililohusisha vijana zaidi ya 4,400 kutoka majimbo yote ya kanisa Katoliki.

“Sasa tunaelekea kwenye uchaguzi  tumefanya ibada maalum ya  kuombea taifa  kuelekea  uchaguzi  mkuu Oktoba 29 mwaka huu ,lakini  aliyeshinda ashinde kwa haki  na atakaye shindwa ashindwe kwa haki ili kuhepuka  migogoro,” amesema.

Amesema Mungu amewapenda na kuwafanya kuwa mashahidi hivyo   watanzania  hususani vijana kutokubali kupokea rushwa  kwani  dunia isiyotawaliwa kwa haki itatawaliwa na shetani.

“Vijana  nyie ni wa thamani kubwa mbele za Mungu na  anawapenda  na amewainua  kuwakomboa kwa damu ya Yesu sio kwa fedha wala dhahabu  ukilitambua hilo utokata tamaa katika maisha ,”amesema.

Amesisitiza  katika kuhitimisha kongamano la sita la vijana kitaifa  amewakumbusha  kutambua  Yesu  anawapenda wakawe  mashahidi wa kutenda haki, ukweli, matumaini kwa kutoa ushuhuda wa imani na  matendo,” amesema.

Amesema, “Uchaguzi  wa mwaka huu suala la haki  likatazamwe kwa upana wake ili kuhepusha  migogoro mingi kwa lengo la kuleta furaha upendo na mshikamano na kuomba  Watanzania kuliombea taifa amani na utulivu.”

“Dunia isiyokuwa na haki ni sawa na  Jehanamu na kumililiwa na shetani, kama Kanisa wamekuwa na  vyombo vya haki na  kutenda haki, lakini pia atakayeshida ashinde kwa haki na atakayeshindwa ashindwe kwa haki,”amesema.

Katika hatua nyingine, amesema asilimia kubwa vijana wanaoingia katika ndoa ni mihemko ya kuiga na  kuwataka kuongeza bidiii katika Dini na kupata mafundisho ya Kanisa.

“Vijana  nunueni vitabu vya mafundisho msome  ili kujifunza na kulisikiliza Kanisa Katoliki ni mama na mwalimu  wa imani endapo ukipata changamoto  za  maisha  ujiulize linasema nini?”amesema.

Katika hatua nyingine ameonya matumizi mabaya ya mitandao ya kijamii na badala yake watumie muda mwingi kusoma biblia ili maisha yawe mema duniani na mbinguni,”amesema.

Mwenyekiti  Taifa wa Vijana Wakatoliki Wafanyakazi (Viwawa), Leonard  Mapolo amesema wamepokea  maagizo yaliyotolewa uongozi  wa kanisa kuombea taifa kutenda kwa misingi ya amani na usawa sambamba  na kupinga rushwa.

“Kwa kuzingatia huu ni mwaka  wa uchaguzi wa kuchagua Rais, Wabunge na Madiwani  tutakwenda kutekeleza maelekezo  kwa kutenda haki licha ya kuwepo  kwa changamoto  ya kiuchumi kwa kundi la vijana,”amesema.

Amesema kwa kipindi kirefu kuna changamoto  ya fursa ya ajira sambamba na kukosekana kwa huku rushwa ikiwa kipaumbele  jambo ambalo linakwamisha vijana wengi kukata tamaa.

 Akizungumza kwa niaba ya Serikali, Mkuu wa Wilaya ya Ileje Mkoa wa Songwe,  Farida Mgomi amewasihi vijana kuwa wazalendo katika  kipindi  hiki kuelekea uchaguzi mkuu Oktoka 29  mwaka huu.