Polisi waanza operesheni kudhibiti magendo, uvuvi haramu Ziwa Nyasa

Mbeya. Polisi Mkoa wa Mbeya kwa kushirikiana  na vyombo vya ulinzi  na usalama wameanza rasmi operesheni  maalumu ya kukabiliana na  kudhibiti  bidhaa za magendo, uvuvi haramu kwa kutumia boti katika Ziwa Nyasa Wilaya ya Kyela.

Hatua hiyo imekuja ikiwa imepita siku moja baada ya Mkuu wa Mkoa wa Mbeya, Beno Malisa  kumkabidhi boti Kamanda wa Polisi Mkoa wa Mbeya, Benjamin Kuzaga kwa niaba ya vyombo vya ulinzi na usalama majini.

Kamanda Kuzaga ametoa kauli hiyo Jumamosi Agosti  23, 2025 baada ya kushuhudia kikosi kazi cha wanamaji  kikianza  rasmi operesheni  ya majini kukabiliana  na uvuvi haramu, usafirishaji bidhaa za magendo katika Ziwa Nyasa.

“Boti hii ni miongoni mwa 11 zilizotolewa na Serikali  ya  awamu ya sita chini ya Rais Samia Suluhu Hassan kwa lengo la kuimarisha  ulinzi wa doria za kudhibiti uvuvi haramu, usafirishaji bidhaa za magendo kutoka nchi jirani,” amesema.




Kuzaga amesema katika kuhakikisha  doria zinazaa matunda vyombo vyote  vya ulinzi na usalama zikiwepo  mamlaka nyingine za Serikali  watashirikiana na Jeshi la Wananchi Tanzania (JWTZ), maofisa Uhamiaji na Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA).

Awali akizungumza baada ya  kukabidhi bodi hiyo kwa  kikosi cha wanamaji katika  Bandari ya  Itungi ,Mkuu wa Wilaya ya Kyela,  Josephine Manase amesema  inakwenda kuimarisha ulinzi katika Ziwa Nyasa kupitia doria na kuifanya wilaya hiyo na Mkoa wa Mbeya kuwa salama.

“Tuna imani sasa shughuli za ulinzi kwenye  ziwa letu zinakwenda kuimarika na kuwa salama hususan  kulinda rasilimali  za Taifa kwa kudhibiti bidhaa  za magendo, uvuvi haramu na matukio  ya uhalifu, “amesema Manase.

Kwa upande wake, Kamanda wa Kikosi cha Polisi Wanamaji nchini, Moshi Sokoro amesema  hiyo  ni miongoni mwa boti 11 zilizotolewa na Serikali  na kugharimu zaidi ya Sh4.5 bilioni.

Kamanda wa Polisi Mkoa wa Mbeya, Benjamin Kuzaga (kulia) akipeana mkono na Mkuu wa Wilaya ya Kyela, Josephine  Manase (kushoto) kama sehemu ya kuzindua  rasmi oparesheni  ya doria  ya  kutumia boti kukabiliana  na usafirishaji magendo, uvuvi haramu katika ziwa nyasa.



Sokoro ametoa kauli hiyo kwa   niaba ya Mkuu wa Jeshi la Polisi nchini ( IGP) Camillus Wambura ameagiza  kikosi cha wanamaji  kuitunza na  kuitumia kwa malengo yaliyo kusudiwa  kuzuia na kudhibiti uhalifu wa majini  bidhaa za magendo, uvuvi haramu na wahamiaji haramu.

Awali Mkuu wa Mkoa wa Mbeya, Beno Malisa, alisisitiza vyombo vya ulinzi  na usalama  kuhakikisha  wanashirikiana kufanya doria  za mara kwa mara ili kukabiliana na matukio  ya uhalifu katika ziwa hilo hususan kwenye fukwe.

Mmoja wa wavuvi na mfanyabiashara  wa samaki, Festo Wille ameshukuru Serikali  kwa hatua hiyo akiamini itarejesha usalama wa uvuvi ziwani humo.