Fyatu ‘kuchangisha’ matrilioni ya kampeni

Japo mie na chata letu tumepiga njuluku za mafyatu hata kabla ya dunia kuumbwa, lazima tuzidi kuwafyatua ili wasitufyatue. Hakuna wakati mzuri wa kufyatua njuluku za mafyatu hasa wale mafisi na mafisadi kama huu.

Kwa vile huu ni wakati wa kupika kura ya kula, lazima wasaka kura ya kula waliwe na wapika kura ya kula. Hapa, ndipo kamchezo ka kufa kufaana huchezwa vilivyo.

Hivyo, mafyatu wangu msinishangae kwa kile nitakachofyatua hapa katika harakati za kufyatua maulaji ya kuwafyatuliwa mafyatu waliogoma kufyatuka wakaishia kufyatuliwa badala ya kufyatuka na kufyatua wawafyatuao.

Kwa vile mie ndiyo dingi hata mungu wao, lazima niwafyatue. Nisipowafyatua, ima watajifyatua, kufyatuka, kufyatua au kufyatuliwa na wengine.

Si mnawajua mafyatu walivyo fyatu hasa kwa vitu visivyo na maana kwao kama kukubali kufyatuliwa wakati wana kila pawa ya kufyatua wanaowafyatua. Hivyo, mjue wazi.

Ninakuja na dili la kuchangisha njuluku kwa ajili ya uchakachuaji, uchafuzi, sorry, uchaguzi mkubwa. Sitajali namna ulivyopata njuluku iwe ni kwa kuuza bwimbwi, ufisadi, au ujambazi, sijali.

Iwe ni malipo ya ngono, sadaka, ujambazi nk, mie sijali. Duniani, hakuna njuluku chafu hata itokane na mambo machafu vipi.

Fyatu sitauliza namna wachangiaji wangu walivyotengeneza njuluku zao. Wewe kama ni fisadi, jambazi, kahaba, tapeli, mpiga ramli nk, lete mchango wako Fyatu aufyatue ushind ili tufyatue ulaji wa dezo pamoja. Njoo tena hadharani bila wasi wasi wowote. Wote wenye maskandali makubwa kama akina IpTL, Kagoda, na wengine, leteni michango yenu ili madhambi yenu yasafishwe kwa ushindi wa Fyatu pale kwenye boksi. Huuni wakati wa madili siyo maadili. Nani aliwahi kula maadili?

Najua yapo mafyatu yanayoshangaa inakuwaje Fyatu mzima na heshima na udhu wangu napwakia njuluku chafu bila kujali zilivyochumwa au kutengezwa kwa madhambi machafu kuliko hata ya ibilisi mwenyewe na Yuda Iskarioti yasijue hawa jamaa bado wamo duniani tena katikati yao. Nani aliona madhabahuni wahusika wakihoji au kushuku watoaji namna walivyopata au kutengeza njuluku hata wawe wanatia shaka namna gani wakati lao moja?

Nani aliwahi kuhoji hizo njuluku zinavyotumika? Mbona wapo wengi wachumao madhabahuni na kwenda kuhonga machangu hata wengine kufunga ndoa za siri?

Kwani, mafyatu hawajui au kwa vile hatuwafyatui? Kiendacho kwa mganga huwa hakirudi wala kurudishwa? Nani aweza kuwa na uthubutu wa kuuliza maswali ya kifyatu kama yangu? Thubutu! Wakifanya hivyo, watakula mafi yao kama Kimarooh aliyekataa kuiba?

Kwa vile ushindi wangu utakuwa ni wa mafyatu wote waliogoma kufyatuka, kutufyatua, na kutuacha sisi tuwafyatue kirejareja, ninachoweza kusema ni kimoja tu.

Nyie mafyatu wakumbaff, leteni njuluku zenu ili nizitumie nishinde halafu ‘niwape’ sorry, mnipe ulaji wa kurejesha njuluku zenu kama zangu.

Nitakuwa nikila nyama wakati nyinyi mkimeza mate na kujilaumu wa kujiruhusu kufyatuliwa mkenge mchana kweupe kana kwamba hamna macho au uwezo wa kufyatuka na kufyatua wawafyatuao. Hamkuambiwa kuwa fedha huleta fedha? Unawafyatua mafyatu baada ya kukufyatua kwenye kipindi cha mchakato kwa miaka metano.

Huku huitwa kufyatuana ambako wanene tunawafyatua wachovu. Nikishinda, tena kwa kishindo, nitaashika patamu ilhali wabaya wangu wakishika au kushikishwa pachungu.

Hapa, lazima watakaonichangia njuluku nao wale utamu kama ninavyokula mimi. We, usicheze na utamu. Japo, mara zote, ahadi huwa vigumu kutekelezeka, kipindi hiki, naapa nitazitimiza hata kwa kutozitimiza, sorry, zote.

Muhimu, kwangu, wachangiaji ni bora na muhimu kuliko wapika kura ya kula makapuku wasio na meno ya kutafuna kaya kama washitiri wangu.

Ukitaka kufaidia maulaji chini ya utawala wangu, changia kampeni zangu. Kuchangia ni bora kuliko kupika kura ya kula.

Sera yangu ni madili siyo maadili. Ijulikane. Sera yangu kuu ni kujihudumia siyo kuhudumia wengine.

Ni kuwatumia na kutumikisha mafyatu na siyo kuwatumikia. Ni kuwafaidi siyo wao kufaidi sera zangu, ni kuvuna nisipopanda. Ni kuchuna na siyo kuchunga.

Kimsingi, sera yangu ni kufyatua siyo kufyatuliwa. Nani anataka kufyatuliwa usawa huu? Mie na genge langu lazima tule kwanza tena bila kunawa wala kuomba.

Huku huitwa kufyatua au kugonga. Lazima ufyatue kabla ya kufyatuliwa; ugonge kabla ya kugongwa.

Tukishinda, lazima tule kwa mikono ni miguu. Najua wabaya wetu wataseme tunakula kama mainzi.

Juzi, nilimsikia adui mmoja akionya mafyatu eti wasinipe kura ya kula kwa vile nitakula na kunonihino humo kama mainzi machafu na mafu.

Hawa wanaonilinganisha na mainzi wangoje niukwae. Watajua kuwa hawajui. Unawezaje kunilinganisha na midudu inayokula na kunonihino na kutapika humo humo? Nawaacha wazoze.

Wajue nikishaula wataula wa chuya kiasi cha kujikuta wakinonihino kwenye debe kwa kashafa hii. Hivi, leo ni siku gani na niko wapi nikiongelea nini?