Kama Mafyatu na wasomaji wangu wote wajuavyo, hiki ni kipindi cha uchakachuaji, sorry, uchafuzi, sorry, uchaguzi. Mbali ya kuwa msimu wa kufyatuana na kufyatuliwa, ni msimu wa kutumia akili vilivyo.
Ni msimu wa kusukuti namna ya kufyatuana mkenge. Wakati mwingine inabidi ujitoe ufahamu ili kuwanasa mafyatu ambao unaweza kuwashtaki kwa kujitoa ufahamu kutaka kufahamu mambo yako.
Juzi hamkumsikia fyatu fulani wa ovyo akijitoa ufahamu na kuwashutumu mafyatu waliomstukia kujitoa ufahamu waliompa vidonge vyake ili kuzuga mafyatu wasijue hujuma anayoifanyia kaya. Kumbe ndiyo maana mzee Nchonga alimshiti!
Kufanikisha dili hili, lazima ukengeuke kama kenge na kuwaacha mafyatu wamchekao kenge kukimbilia mtoni mvua inyeshapo wasijue anajua sayansi kuliko wao. Maskini, mafyatu, pamoja na wengine kuwa na PhD ziwe feki, kweli, au heshima, hawajui kuwa maji ya mto ni ya uvuguvugu kuliko ya mvua nyakati za asubuhi na mvua zikiwa zinanyesha! Ajabu, kenge hajasomea shahada wala kupewa lakini anayajua haya.
Pamoja na kufundishana sayansi, mafyatu bado hawalijui hili hadi wanamcheka kenge wakati makenge ni wao wa kuchekwa kwa ujinga na ulimbukeni wao kujicheka bila kujua. Kwa sababu kenge ni mjanja na mjuzi, huwa hapotezi muda kuwacheka wala kufanya uzwazwa wao wa kujitoa ufahamu kama wao.
Juzi, baada ya kumaliza kuchangisha michongo, sorry, michango kwa ajili ya uchaguzi, sasa lazima nitafute namna nyingine ya kufyatua viti vyote tena kwa kishindo hata iwe ni kwa goli la mkono. Kwa ufupi, huu ni msimu wa kutia nia, kuonyesha nia za ufyatuaji. Hivyo, mimi ninakuja na mkakati kabambe mwingine wa kuhakikisha nashinda viti vyote. Nina sera ya KUBIKU, yaani Kupita Bila Kupingwa.
Kwa kutumia kanuni na sera ya KUBIKU, nitahakikisha kuwa nashinda kwa kishindo hata kama nitashindwa ili wanaojaribu kunishinda niwashinde kwa kishindo. Baada ya kujihakikisha ushindi, nahakikisha na Bi Nkubwa wangu, vitegemezi, maswahiba, hata waramba manonihino yangu lazima wanapitishwa bila kupingwa. Atakayejitia kiherehere cha kunipinga au kuhoji lolote kuhusiana nami nilivyowaburuza mafyatu na kujiteua kugombea unene, ajiandae kupigwa chini bila kumuangalia usoni.
Ukitaka kumfyatua nyani, waambwa, usimuangalie usoni. Mie huwa namuangalia makalioni na kuwachoma mkuki. Tuendelee.
Huu ndiyo mpango mzima ambao umefanyiwa utafiti katika kaya nyingi zilizocheza na kutumia kamchezo haka.
Kwanza, nitahakikisha hata bata, kuku, mbwa, na paka wanapita bila kupingwa chini ya sera ya KUBIKU.
Hii inaitwa demoncracy ambapo maruhani, mapepo wachafu, hata wadudu hushirika. Hii huwa na maana ikizingatiwa kuwa kuna mafyatu wanaonichukia wanaosema eti namna mafyatu wanaovyonichukia, hata nikigombea na chawa waliojaa kitandani mwangu, nitashindwa. Hashindwi fyatu hapa. Kawaulize wale waliojitia kujiondoa kwenye chata chetu na kuanza kunitupia matope. Wameshindwa.
Na punde, wataregea na kutoweka. Mifyatu mingine, nadhani inahitaji kukutana na wale wasiojulikana wanaojulikana kwa uanimo wao. Wangejua ninao mtandao mkali wenye historia ndefu katika kaya hii, wasingejaribu hata kunung’unika achia mbali kupayuka na kuzoza. Kama ni wajanja, si wafyatuke niwafyatue kama ninavyowafyatua mafyatu waliogoma kufyatua na kutufyatua hadi tukawafyatua kila baada ya miaka mitano tutakavyo.
Nina hasira na namna wajumbe walivyotufyatua wasijue nasi tutawafyatua tena kwa miaka mitano fresh.
Pili, nilifanya uchaguzi wa ndani ya chama cha Mafyatu (ccM). Guess what? Mafyatu wote walioonyesha kutishia ulaji wangu na washikaji zangu walipigwa chini na kuanguka kama mende. Sina simile na yeyote anayejitiatia. Lazima nifyeke wote wanaotishia ulaji wetu hata wawe binadamu, chawa, au mafyatu. Nilihakikisha wanakatwa kinoma ili wasituletee noma kinomi. Wanaotaka kuendelea na ukumbaff huu wa kuhoji nitakavyojipitisha kuwa mgombea wa chata letu bila kufuata katiba na utaratibu, wajiandae kwa kiama kitakachowakumbwa soon.
Tatu, lazima niongee na washikaji wangu walioko kwenye NGOs za kusimamia uchakachauaji kuwapiga chini viherehere wanaotaka kushindana nami. Hao, wajiandae. Nao kiama chao kinakuja.
Nitahakikisha wanapigwa chini hata kwa kupinda sheria.
Nne, nitahakikisha vibaraka wangu na vyata vyao vya mfukoni ambavyo vinaishi kwa kutegemea hisani yangu wanaingia kwenye kinyang’anyiro kama boya la kunipinga wakati lao moja. Kwa vile muda hautoshi, naachia hapa. Nakwenda kuandaa mikakati ya kushinda kwa kishindo hata kama itahitaji kujitoa ufahamu na kuchakachua kura za mafyatu walikataa kufyatuka na kulinda kura zao.
Sijui ni kwa sababu hawajui kuwa kura ni mali. Nadhani hawajui kuwa kura ni zana ya kula tena dezo na kutanua bila kufyatuliwa na yeyote kwa vile inakuweka juu ya sharia.
Sijui ni kwanini mafyatu hawajui kuwa ukitumia vibaya kura yako unafyatuliwa hata kuliwa! Nadhani tatizo ima ni kujitoa ufahamu au ukenge makengeza wa kutojua thamani ya kura. Amani, kura ni kula ila kula si kura. Mbona rahisi hivi? KUBIKU hoyeee!! Du! Kumbe bangi imenitoa ufahamu!!!!!!