RC Malisa aagiza maofisa kusimamia asiyepanda miti 20 kunyimwa kibali cha ujenzi

Mbeya. Mkuu wa Mkoa wa Mbeya, Beno Malisa amewaagiza maofisa mazingira, ardhi na mipango miji kuweka utaratibu mzuri utunzaji wa mazingira na kutoruhusu mtu kujenga pasipo kupanda miti 20 katika maeneo yao.

Hatua hiyo imetajwa kuwa sehemu ya kuhamasisha jamii katika utunzaji wa  mazingira  kwa kutambua ni  jukumu la kila mmoja na  sio kwa vikundi  wala Serikali.

Malisa ametoa agizo hilo wakati akikabidhi hundi  ya Sh40.5 milioni kwa vikundi 18  vya kuweka na kukosa na utunzaji wa mazingira  Mkoa wa Mbeya.

Mkuu wa Mkoa wa Mbeya,Beno Malisa(kulia) aliwa ameshika hundi ya Sh 40.5 milio ambayo alikabidhi kwa vikundi vya kuweka na kukopa na utunzaji  wa Mazingira  Mkoa wa Mbeya(katika) Meneja mradi  wa Shirika  la Likolto, Shukuru Tweve

Hundi hiyo imekabidhiwa kwenye mkutano maalumu ulioandaliwa Shirika la Likolto na kufanyika katika Ukumbi wa Beaco jijini na kuhusisha baadhi ya halmashauri.

“Mtu asipewe kibali cha ujenzi mpaka  apande miti 20 katika eneo lake, lakini maofisa mazingira, ardhi  na mipango miji wekeni  utaratibu  mzuri wa utunzaji wa mazingira,”amesema Malisa.

Malisa amesisitiza jukumu la kutunza mazingira ni la kila mmoja na sio vikundi wala Serikali na kwamba anayehitaji kuishi lazima ajikite kutunza mazingira.

“Maofisa wa Serikali  msitoe vibali wala  kuruhusu  mtu  kujenga pasipo kupanda  miti, lakini pia wekeni utaratibu mzuri wa kutoa elimu kwa jamii na kujua umujimu wa  utunzaji wa mazingira,” amesema Malisa.

Kuhusu hundi iliyotolewa, Malisa ameagiza Shirika la Likolto na wanufaika kuhakikisha zinatumika kwa malengo yaliyo kusudiwa na sio vingine.

“Niwaombe zingatieni matumizi ya fedha mlizopata katika kuunga mkono jitihada za Serikali ya awamu ya sita chini ya Rais Samia Suluhu Hassan katika suala la utunzaji wa mazingira ili kuifanya Tanzania hususani Mkoa wa Mbeya kuwa kijani,”amesema.

Msimamizi wa Mradi kutoka Shirika  la Likolto, Shukuru Tweve  amesema lengo la kutoa  ruzuku  hiyo ni kuwekeza  utunzaji wa mazingira  kwa kupanda  miti ya matunda, mbogamboga  na kuboresha makorongo ya mito yaliyo athirika na mmonyoko wa udongo.

“Vikundi vilivyo nufaika mikoa ya  Mbeya na Songwe vitakwenda kuongeza  nguvu  utunzaji wa mazingira, upandaji wa miti rafiki ya matunda  na mbogamboga na kuhifadhi maeneo  yenye makorongo,”amesema Tweve.

Amesema  kupitia mradi huo vikundi 18 kutoka  Mkoa wa Mbeya vimenufaika na  ruzuku  ya Sh40.2 milioni na Mkoa wa Songwe vikundi 10 vitanufaika na ruzuku ya Sh22.5 milioni.