Mgombea ubunge Patali aomba kupandishwa hadhi Mbalizi akiomba kura za Rais

Mbeya. Mgombea urais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa tiketi ya  Chama cha Mapinduzi  (CCM), Samia Suluhu Hassan ameombwa atakapoingia madarakani kupandisha hadhi mamlaka ya Mji wa Mbalizi Wilaya ya Mbeya ili kuboresha shuguli za kiuchumi.

Ombi hilo limetolewa leo Alhamisi  Septemba 4, 2025  na mteule wa ugombea ubunge wa Jimbo la Mbeya Vijiji, Patali  Shida ambayo pia iliungwa mkono na aliyekuwa mgombea ubunge Jimbo la Rungwe, Sophia Mwakagenda.

Awali, mgombea  Jimbo la Mbeya, Patali amesema Serikali ya awamu ya sita kwa kipindi cha miaka minne imefanya mambo  makubwa hususani kutenga  zaidi ya Sh6 bilioni kwa ajili ya kutekeleza miradi  mbalimbali hususani  katika sekta ya afya.


Amesema Jimbo la Mbeya Vijijini tangu kuanzishwa kwake mwaka 1980 haikuwahi kupata Hospitali ,lakini kwa kipindi cha miaka minne ya uongozi wa Rais Samia  wamepata fedha kwa ajili ya  ujenzi  wa vituo vya afya sita na zahanati 10.

“Mgombea urais tumepata zahanati 10 vituo vya afya sita jambo ambalo limeboresha upatikanaji  wa huduma bora za afya zikiwepo za mama na mtoto wakati  wa kujifungua,” amesema.

Katika hatua nyingine Patali amesema  asilimia  85 ya wananchi Mbeya Vijijini wanajihusisha na shughuli za kilimo huku  jumla ya wananchi 110,000 wamesajiliwa kwenye mfumo wa mbolea na mbegu za   ruzuku.

“Wilaya ya Mbeya mahitaji ya chakula ni  tani  200,000, lakini uzalishaji  wetu mpaka sasa hivi ni tani 600,000 haya yote ni uwekezaji wa Serikali ya awamu ya sita na utekelezaji  wa ilani ya Uchaguzi  2020/25,” amesema.

Patali amesema mbali na mafanikio hayo wanashukuru kwa maelekezo ya ujenzi wa barabara njia nne hali ambayo itaokoa maisha ya watanzania yaliyokuwa yanakatishwa katika mteremeko wa mlima Iwambi na kupunguza  foleni.

Patali amesema kufuatia mamlaka hiyo kuwa ndogo  amemuomba Rais Samia kama ikimpendeza  wakati michakato ikiendelea ya kupitia halmashauri zitakazo pandishwa hadhi  Mamlaka ya mji mdogo  wa Mbalizi ipewe kipaumbele.

“Mh Rais ukitazama mji wa Mbalizi na maendeleo yaliyopo,unatuletea barabara njia nne na Uwanja wa Ndege wa Songwe na  viwanda  vidogo, tunaomba ikikupendeza pandisha hadhi  mji huu ili tukutendea haki,”amesema.

Ombi hilo limeungwa mkono na aliyekuwa mgombea  jimbo la Rungwe, Sophia Mwakagenda ameomba mji huo uwe kamili kutokana na kuwa na Mamlaka ya kubariki ombi lao.

“Wanambalizi Oktoba 29, 2025 tukampatia kura za kishindo Rais Samia Suluhu Hassan, lakini ninaamini umebakisha kuapishwa mengine unafanya kama taratibu za kiuchaguzi,”amesema.


Mfanyabiashara wa viazi mviringo  amesema endapo Serikali ikaridhia kupandisha hadhi mamlaka hiyo shughuli za kiuchumi zitatanuka na kuchochea mapato ya Serikali.

“Tunaona Mji wa Mbalizi unatanuka kila wakati hususani  shughuli za kiuchumi  na kilimo nasi tunaunga mkono kauli ya mgombea  ubunge wetu mwenye maono ya kuleta maendeleo ya kweli,”amesema.

Katika hatua nyingine wameomba kuboresha  miundombinu  ya barabara za pembezoni  ili kurahisisha  kusafirisha  mazao kutoka sehemu mija kwenda nyingine, “amesema.

Akihutubia wananchi wa Mamlaka ya Mji wa Mbalizi  Wilaya ya Mbeya,  mgombea  urais Samia Suluhu Hassan amesema suala hilo liko kwenye mchakato litapita Tamisemi na wakipika serikalini wataangalia la kufanya.