NA EMMANUEL MBATILO, MICHUZI TV
Baraza la Taifa la Hifadhi na Usimamizi wa Mazingira (NEMC) limezindua kampeni ya kitaifa ijulikanayo kama “NEMC Usafi Campaign” yenye lengo la kuhamasisha jamii kushiriki kikamilifu katika shughuli za usafi na uhifadhi wa mazingira kwa ajili ya kizazi cha sasa na kijacho.
Akizungumza na waandishi wa habari wakati wa uzinduzi huo, Kaimu Mkurugenzi wa Uzingatiaji na Utekelezaji wa Sheria wa NEMC, Jamal Baruti, amesema kampeni hiyo inalenga kuunganisha nguvu za jamii katika kuhakikisha hifadhi endelevu ya mazingira.
“Malengo yetu ni makubwa lakini yanawezekana. Tunataka kufikia angalau asilimia 80 ya kaya kushiriki shughuli za usafi ifikapo Desemba 2025, kupunguza utupaji wa taka ovyo mijini na vijijini, na kuzigeuza taka kuwa fursa ya kiuchumi,” amesema Baruti.
Aidha amesema kuwa suala la hifadhi ya mazingira limepewa kipaumbele katika Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050, inayolenga kujenga Tanzania yenye jamii inayotunza na kulinda mazingira.
Kwa mujibu wa takwimu zilizotolewa, Watanzania huzalisha kati ya tani milioni 14.4 hadi 20.7 za taka ngumu kwa mwaka, sawa na kilo 0.66 hadi 0.95 kwa kila mtu kwa siku.
Kwa upande wake, Afisa Mazingira Boniface Kiaruzi alisema kuwa taka ni fursa, na kupitia kampeni hiyo wananchi watapatiwa elimu kuhusu utunzaji wa mazingira, urejelezaji wa taka na namna taka zinavyoweza kutumika kama rasilimali ya kiuchumi.