MCHENGERWA AZINDUA KAMPENI ZA UDIWANI MSASANI, MWANANYAMALA. AMWOMBEA KURA RAIS SAMIA

Na Mwandishi Wetu 

Mjumbe wa Halmashauri Kuu Taifa CCM kuipitia Mkoa wa Pwani, na Waziri wa TAMISEMI, Mhe Mohamed Mchengerwa amewaomba watanzania  kumpigia kura zote za ndiyo Rais Samia Suluhu Hassan kwa kuwa amefanya kazi kubwa ya kuwaletea watanzania maendeleo. 

Mhe. Mchengerwa ametoa rai hiyo leo alipokuwa mgeni rasmi katika uzinduzi wa kampeni za udiwani katika kata za Msasani na Mwananyamala jijini Dar es Salaam.

 

Akimtambulisha na kumnadi mgombea wa udiwani wa kata ya Msasani Yusufu Hamisi  Yusufu amesema kata ya Msasani ni ngome  ya Chama Cha Mapinduzi (CCM) toka enzi za Mwalimu Nyerere hivyo wananchi hawana budi kulinda heshima hiyo kwa kukipigia kura za ndiyo Chama hicho katika ngazi zote kuanzia  urais, ubunge na udiwani.

“Ndugu zangu naomba tunapoelekea kwenye uchaguzi mkuu tusibabaishwe, tuungane  kupiga kura zote za ndiyo kwa Rais Samia, wabunge na madiwani wa CCM ili tuendelee kuboresha maisha ya watanzania.” Amesisitiza Mhe Mohamed Mchengerwa 

Aidha, amewasihi wananchi kumchagua mgombea wa udiwani wa kata hiyo kwa tiketi ya CCM ndugu Yusufu huku akisisitiza kuwa mtu hodari na mtendaji zaidi kuliko maneno.

Akiwa Mwananyamala Mhe. Mchengerwa amewaomba  wananchi wa kata hiyo kumchagua aliyekuwa diwani na Meya wa Kinondoni ndugu Songoro  ili aendelee kuwaletea maendeleo pale alipoishia.

Amesema kutokana na uchapakazi wake ndiyo maana pia aliweza kuchaguliwa kuwa Meya wa Kinondoni hivyo hana shaka kuwa hata kipindi hiki atarejea katika kiti hicho.

Amewasihi wananchi kuachana na siasa zisizo  za maendeleo na badala yake kukipigia kura  CCM kwani tayari kimeshawafanyia mambo makubwa ya maendeleo wananchi kupitia kwa Rais Samia Suluhu Hassan.

Ametaja baadhi ya maeneo makubwa yaliyopatikana katika kipindi hiki kuwa ni pamoja na kuimarika kwa miundombinu, SGR, kukamilika kwa bwawa la Mwalimu Nyerere, Elimu pamoja na Afya.

Msanii chipukizi  wa Singeli nchini, Dogo Paten ametumbuiza na kukonga nyoyo za wananchi waliojitokeza kwenye uzinduzi wa Kata ya Msasani.