Dk Tulia aahidi kutatua kero za wananchi Uyole, kutekeleza ilani ya CCM

Mbeya. Wananchi  Kata ya Ilomba Mkoa wa Mbeya,  wamemtaka mgombea  ubunge  Uyole,  Dk Tulia Ackson kuondoa adha  ya maji, ujenzi wa kituo cha afya na vumbi kwenye barabara za mitaa huku naye akisema kero zao atazifanyia kazi akishinda uchaguzi mkuu.

Awali akiomba kura za Rais na wabunge  na madiwani  kwa wananchi, Mzee wa Mila, Chifu Adamson Kipingu amesema wakati wa porojo umepita sasa wanahitaji maendeleo.

Mkazi wa Ituha Selina Hamis,  amesema ili kuhakikisha mgombea nafasi ya Rais na ubunge likiwepo la Uyole wanapata kura za kishindo  kama wanawake na makundi  maalumu  kazi ni moja kusaka kura na kutiki Oktoba mwaka huu.

“Tumeona maendeleo ya Mbeya Mjini  nasi huku Uyole  tunahitaji  tumekosa kwa miaka mingi hususani  barabara, maji na ukosefu wa kituo cha afya,” amesema.

Amesema kimsingi wameona utekelezaji  wa ilani ya uchaguzi  2020/2025 sasa wanampa kibarua mgombea  ubunge Uyole  Dk Tulia  akipata ridhaa  kuanza na kipaumbele  cha barabara, maji na ujenzi wa kituo cha afya Kata ya Ilomba   ikiwa ni sehemu ya kutekeleza  ilani ya uchaguzi 2025,2030.

Akiomba kura kwa wananchi wa Kata ya Ilomba,   Katibu wa Siasa na Uenezi Wilaya ya Mbeya, Philimon Mng’on’go amesema anaona jinsi  Uyole itakavyo kimbia kimaendeleo, lakini tunajua kuna upinzani tuombe Oktoba  29, 2025  wampigie kura mgombea ubunge Uyole Dk Tulia na Rais Samia Suluhu Hassan.

“CCM tunahitaji  ushindi wa heshima  kina mama, kina baba wakati ukifika  jitokezeni  kupiga kura za heshima za Rais Samia na Dk Tulia kama kurejesha shukrani ya maendeleo yaliyoletwa kwa miaka mitano, “amesema.

Mgombea udiwani Kata ya Ilimba, Noah Mwakisu amesema kauli hizo za wananchi kupigia kura CCM ni  kutokana na maendeleo yaliyoletwa na Serikali kipindi  cha miaka mitano.

Pia, ameomba  kutatuliwa changamoto  ya ubovu wa  barabara,maji na ujenzi wa kituo cha afya ili kusogeza  huduma  jirani hususani  kwa wakinamama wajawazito.

“Kata yetu ina wananchi  40 ,000 lakini hatuna kituo cha afya, huduma  ya maji  safi ya uhakika na barabara  zetu ni vumbi ombi letu Serikali  ilione hilo na kusisitiza  wananchi kupiga kura za kishindo  Oktoba  mwaka huu ili maendeleo  kufikiwa na miradi ,”amesema.

Dk Tulia amewaondoa hofu wananchi na kwamba CCM  wamejipanga kuleta maendeleo Uyole.

“Akija mtu akikupa habari za Dk Tulia waelezeni tumeishi naye, lakini wana Ilomba mmeona kazi tulizofanya  CCM Uyole tumejipanga,”amesema.

Amesema mwakani kuna wanafunzi watajiunga kidato cha kwanza na Serikali  imeweka mazingira  mazuri na wezeshi  hakuna changamoto ya madawati, madarasa.

Amesema mbali na uwekezaji  wa Serikali  sekta ya elimu kama mgombea ubunge wa kujiongeza  ifikapo Januari  mwaka 2026 , watoto  walio chaguliwa  kujiunga kidato cha kwanza katika kaya zisizojiweza  watapewa sare za na mahitaji mengine bure lengo watimize ndoto zao za kupata elimu bora.

Amesema Serikali  itaendelea  kuboesha miundombinu  hususani ujenzi wa vituo vya afya ikiwepo utekelezaji  wa ilani ya uchaguzi  2020/2025 ya ujenzi wa  miundombinu  ya jengo la ghorofa katika  Hospitali ya Rufaa  Kanda  kitengo cha wazazi  Meta kwa gharamu ya Sh11 bilioni ambayo imeanza kutoa huduma.

“Lakini pia  tunakuja na utekelezaji  wa sheria ya bima ya afya kwa wote ambayo  itaanza hivi karibuni sambamba na yeye binafsi  kuendeleza kutoa  bima za afya kwa Kata 13 za Jimbo la  Uyole,”amesema.

Amesema  wana Uyole wana bahati kuna ujio wa  mradi wa maji  Mto Simba  sambamba na utekelezaji  wa mradi mkubwa wa  kimkakati wa  chanzo cha mto Kiwila  Wilaya ya Rungwe.

“Lakini pia niwahakikishie  kero ya barabara za mitaa zitatatulia kazi yenu sasa ni kuchagua mafiga matatu Oktoba  29, mwaka huu hususani mgombea urais, wabunge na madiwani,” amesema.