Msituulize tulipopata njuluku tulizowekeza uchaguzini

Siku hizi za uchafuzi, sorry, uchakachuaji, sorry, uchaguzi, tutaona mengi. Yote cha mtoto. Kinachomfyatua na kumtisha Fyatu na ujeuri na ushujaa wake akatetemeka ni makufuru yanayofanywa na vitegemezi vya makapuku wa kunuka, tena vilivyozaliwa jana.

Kama hutapiga selfie na chopa au mindinga ya bei mbaya au wanene uchwara ambao wengi wanatia shaka kuhusiana na udhu wao mwaka huu, ujue una matatizo kiakili.

Hata hivyo, mambo mengine yanaudhi we acha tu. Juzi, katika pitapita zangu si nikakutana na vibaka wa kisiasa wa kisasa wenye visanga na visasi! Si niliahidiwa mshiko ili nikubali kupakizwa kwenye mindinga yao niende kuhudhuria na kushangilia ahadi za urongo urongo na uzwazwa.

Kwanza, kuna kitu kiliniudhi kiasi cha kutaka kufyatuka peke yangu na kuwafyatua mafyatu vibao. Kwa nini kubebwa na mindinga wakati wao wanatesa na chopa? Kwa utapeli na uzwazwa wao walidhani naweza kuhongwa viji-Tshirts, na bi Nkubwa wangu khanga tuwape kura zetu watufyatue kwa miaka mitano ijayo? Siye si chawa, funza, kunguni, wala ruba. Tuna akili tena zinazochemka kuweza kujua na kustukia huu ujambazi uliohalalishwa kwa kisingizio cha siasa.

Pili, baada ya kushuhudia huo ukumbaff, niliamua kuwafyatua hawa majizi wa kisiasa. Hivyo, nawashauri mafyatu mazwazwa wanaoshabikia, kushobokea na kupwakia rushwa hizi ambazo kimsingi, ni njuluku zao zilizopigwa na hawa majambizi wa kisiasa, kuacha kujitia vitanzi wenyewe.

Kwa nini msiwaulize hizo njuluku za kukodisha chopa na ndinga, kumwaga mabango mengine ya kujikomba wamezipata wapi kwenye kaya kapuku kama hii au ni za bwimbwi?

Tatu, waulize. Wananunua nini ili kupata nini? Watazirudishaje kama siyo kuchuuza roho za mafyatu au kufyatua njuluku zao kwa kupewa rushwa na wawekezaji ambao nao si wawekezaji kitu bali wachukuaji?

Nne, watakaopwakia jinai hii wasilie watakapofyatuliwa na kujikuta wakisota kwa maisha magumu. Hii ni shida ya kujitakia. Nachukia mafyatu yanayofikiri na kutenda kama mafisi.

Wakati mwingine, najiuliza. Hivo vichwa visivyotumika walipewa vya nini? Fisi ukimtupia nyama ya fisi mwenzie, anaramba. Panya kadhalika.

Kuku ndo usiseme. Ni aibu na hatari kwa mafyatu kulishwa nyama ya wenzao kwa mlango wa nyuma. Hiyo, njuluku mnayoshobokea ni jasho lenu. Ni yenu.

Tano, hawa wanaohonga ni wahalifu mnaopaswa kuwafyatua wakaishia hata kuzikwa lupango. Hao wanaowahonga wengi ni vitegemezi vya wazazi makapuku tena wa kunuka.

Ukiwaona hawa wanaokodisha chopa, wazazi wao hata wakiona picha ya chopa hawawezi kujua ni nini zaidi ya kuiamkia na kujua Sir God amewatokea tokana na kutowahi kuiona. Sijui hii inasababishwa na ubinafsi, ufisi, ukatili, upofu, au uzwazwa?

Sita, najisikia kupagawa kuona hata lisrikal, we koma, likiwafumbia macho majizi haya ya kisasa ya kisiasa.

Je hii, kwa wenye akili tu, inawafundisha nini? Je jinai ndiyo sera za kisasa? Hawa wahongaji njuluku zetu, wakituuza, tutawalaumu au kujilaumu?

Kura yako siyo njugu ugawa bure bila kujua atakayeliwa ni wewe kwa vile kura hailiwi bali kuwawezesha walaji kula tena dezo. Je, wale wanaoshabikia huu wizi nao si wezi wasio na cha kuiba au kutamani nao wangepata fursa wafyatue na kupiga? Namna hii, kaya itasonga mbele au kuendelea kuwa nyuma?

Saba, acheni ufwala, ulimbukeni, na uzwazwa, na uvivu wa kufikiri. Fyatu fisadi linachezea fedha kwenye madude msiyoweza kuyagusa na kuwakoga, nanyi, kwa ufwala wenu, mnalishangilia badala ya kulizomea na kushinikiza liondolewe kwenye orodha ya wagombea.

Mnashangilia mateso yenu. Wangapi wamewahi au watawahi kupanda chopa? Badala ya kumnyonyoa, mnajirahisisha anawanyonga.

Mkiitwa wanyonge mkanyongea na kunyongwa, mtalalamika au kumlaumu nani? Kweli mafala ndiyo wafyatuliwao!

Nane, hebu tujiulize kifyatufyatu. Hivi, hawa wanaotuaminisha kuwa wana sera na siyo sura (teana za kiwivi) za kutukomboa wana mpango wowote wa maana? Kama wanao, mbona hawaoni haya ambayo Fyatu nayaona ambapo mafyatu wanafyatuliwa kirahisi na kirejareja kana kwamba kaya haina mwenyewe au ni shamba la chizi? Usawa huu, kama tukitumia akili ya comonsense sawasawa, nani anaweza kupata njuluku ya kukodi chopa tena kwa kampeni na siyo kumuwahisha mgonjwa hospitali tena kijana mdogo ambaye hata muda wake wa kufanya kazi haufikii miaka ishirini?

Jamani, tunawafyatua mafyatu kwa sababu waligoma kutufyatua hivyo, tunawaadhibu kwa kuwafyatua tusijue tuifyatua kesho yao na yetu. Kama mafyatu wangejitambua, nadhani swali la kwanza lingekuwa ni kutaka kujua hii njuluku imepatikana wapi, wananunua nini, na watairejeshaje.

Pia, wangehanikiza wafujaji wa njuluku waondolewa. Na mwisho, wangependa kujua sera za wahusika badala ya kushabikia sura.