Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam Mhe. Albert Chalamila ameiagiza Mamlaka ya Majisafi na Usafi wa Mazingira Dar es Salaam (DAWASA) kufuatilia hali ya upatikanaji wa huduma ya majisafi katika maeneo mbalimbali ya Mkoa wa Dar es Salaam pamoja na kuweka mikakati ya haraka ya kuboresha huduma hiyo.
Mheshimiwa Chalamila ametoa maelekezo hayo wakati wa kikao kifupi na Watendaji wa DAWASA cha kufanya tathmini ya hali ya upatikanaji wa maji kwa kubaini maeneo yenye changamoto ya maji kwa muda mrefu ili kutatua na kuboresha huduma ya maji.
Amesema kuwa Serikali imefanya uwekezaji mkubwa katika sekta ya maji kwa kutekeleza miradi mikubwa ya maji ikiwemo mradi wa maji Dar es Salaam ya Kusini (Bangulo) ambao umekamilika na kuanza kutoa huduma katika maeneo ya Segerea, Kinyerezi, Kibamba na Ubungo ambayo awali imekuwa na changamoto ya maji kwa muda mrefu.
“Nikiri kweli kuna maeneo mengi ya Dar es Salaam ambayo yanakabiliwa na upatikanaji mdogo wa maji, nitoe rai kwa wananchi wa maeneo hayo kuwa na subira wakati Serikali kupitia DAWASA ikichukua hatua za haraka za kuhakikisha huduma inaboreshwa.” amesema Mhe. Chalamila.
Amesema kuwa hatua nyingine ambayo Serikali inachukua ni pamoja na matumizi ya maji ya visima zaidi ya 190 vilivyopo kwenye maeneo mbalimbali Dar es Salaam na tayari DAWASA imeanza haraka kutumia visima hivyo kwa lengo la kuongeza kasi ya upatikanaji wa maji.
Kwa upande wake Afisa Mtendaji Mkuu wa DAWASA Mhandisi Mkama Bwire amesema kuwa Mamlaka imepokea maelekezo kutoka kwa Mkuu wa Mkoa na kazi kubwa inaendelea kutekelezwa na Mamlaka kwa lengo la kuboresha huduma.
Amesema kuwa kwa sasa katika eneo la huduma la DAWASA mahitaji ya maji kwa wananchi yameongezeka kwa kiasi kikubwa hadi kufikia mita za ujazo 685,677 kwa siku kutokana na ongezeko la watu mjini, ilihali uzalishaji wa maji kwa siku ukiwa mita za ujazo 534,600.
Amesema kuwa jitihada kubwa zimefanyika na Serikali kwa lengo la kuimarisha upatikanaji mkubwa wa huduma ikiwemo utekelezaji wa mradi wa maji Bangulo unaotoa huduma kwa wakazi wa Segerea, Ukonga, Kisarawe, na maeneo ya Kinyerezi yaliyokuwa na changamoto ya huduma hapo awali.