BALOZI MULAMULA – TUSICHEZEE AMANI, TUKEMEE KWA NGUVU ZOTE VIASHIRIA VYA VURUGU


:::::::::

MJUMBE Maalum wa Umoja Wa Afrika kuhusu Ajenda ya Wanawake, Amani na Usalama, Balozi Liberata Mulamula amesisitiza wananchi kulinda amani kuelekea uchaguzi Mkuu utakaofanyika Oktoba 29, mwaka huu.

Ameyasema hayo, katika mkutano wa Kampeni uliofanyika Jimbo la Kibamba, Wilaya ya Ubungo jijini Dar es Salaam, huku akiwasisitiza wananchi kuwapigia kura wagombea wa CCM wakiongozwa na Dk.Samia Suluhu Hassan na Angela Kairuki.

“Nchi yetu imekuwa ikisifika ulimwenguni kote kama nchi ya amani na usalama. Tusichezee na kuharibu amani yetu hii hususan tunavyoelekea uchaguzi mkuu ambayo imekuwa tunu ya Taifa letu.

“Jukumu la kuimarisha amani yetu ni letu sote kama wananchi, mkubwa na mdogo na viongozi wetu wote. Tukipoteza amani yetu ambayo imejengwa na waasisi wa Taifa hili tangu uhuru, ni vigumu kuirudisha,”alisema.

Alisema amani ikipotea athari zake ni kubwa sana ikiwemo uharibifu wa uchumi, miundo mbinu, huduma za jamii zinateketea ikiwemo hospitali, shule, barabara, kunakuwa na wimbi la wakimbizi wa ndani na nje, wananchi wanakimbia ovyo na kuhatarisha maisha yao na kuishi katika mazingira magumu. 

“Mimi binafsi kama Mjumbe Maalum wa Umoja wa Afrika kuhusu masuala ya amani na usalama ya Wanawake na kama Mtanzania, wito wangu au rai yangu ni kwamba vitendo vyote vyote vinavyoashiria kuhatarisha amani yetu vikemewe kwa nguvu zote hususan katika kipindi hiki tunavyoelekea uchaguzi mkuu,”alisema.

 Alieleza kuwa Tanzania ina historia nzuri ya kuwa na uchaguzi wa amani na haki ambayo inajivunia akizunguka nchi nyingine barani Afrika zilizokumbwa na migogoro na vita. Tusiharibu historia hii. Amani ni urithi, si kitu cha kupoteza, ni zawadi ya vizazi.” 


00000