::::::::::::::
Wazee kupata matibabu bure kupitia kambi ya
MOI Dar es Salaam
Na Mwandishi Wetu
TAASISI ya Tiba ya Mifupa na Ubongo Muhimbili (MOI) itakuwa na
kambi maalum ya uchunguzi na ushauri wa kitabibu kwa wazee, itakayofanyika
kuanzia kesho, Oktoba 16 hadi 18, mwaka huu 2025, katika viwanja vya Mnazi
Mmoja jijini Dar es Salaam.
Kwa mujibu wa taarifa iliyotolewa na Meneja wa Uhusiano wa MOI, Patrick Mvungi,
huduma zitakazotolewa katika kambi hiyo zitahusisha uchunguzi na matibabu ya
kibingwa na kibobezi katika maeneo mbalimbali ikiwemo mifupa, ubongo, mgongo,
mishipa ya fahamu, pamoja na huduma za mazoezi tiba na ushauri wa lishe.
Mvungi amesema lengo la kambi hiyo ni kuboresha afya za wazee na kuwawezesha
kupata huduma bora za kitaalamu kwa urahisi zaidi.
“Huduma hizi zitakuwa bure kwa wazee wasio na bima ya afya, huku wenye bima
wakihudumiwa kwa kutumia bima zao kama kawaida,” amesema Mvungi.
MOI imewataka wazee kujitokeza kwa wingi katika kambi hiyo ili kunufaika na
fursa hiyo adhimu ya kujitunza kiafya.