Na Yohana Kidaga- Muhoro, Rufiji
Mgombea wa Ubunge Jimbo la Rufiji, Mhe. Mohamed Mchengerwa ametoa wito kwa Wanarufiji na Wandengereko wote duniani kufika Rufiji kumpokea mgombea wa Urais wa CCM, Dkt Samia Suluhu Hassan kutokana na kazi kubwa aliyowafanyia katika kipindi chake.
Kesho, Oktoba 20, 2025 Rais Samia Suluhu Hassan na Mgombea wa Urais wa CCM anatarajia kufanya mkutano wa hadhara kuomba ridhaa ya kuchaguliwa katika viwanja vya Ikwiriri.
“Ndugu zangu naomba nitoe wito kwa Wanarufiji na Wandengereko wote duniani kufika kumpokea shujaa wetu na Rais wetu kipenzi ili tumpe shukrani zetu kwa mambo mengi aliyotufanyia kwenye Wilaya yetu. Na asitokee wa kukosa fursa hii”. Alisema Mhe. Mchengerwa mara baada ya kuombewa dua na wazee wa mila na kukabishiwa zana za mila na jadi kuwa Kiongozi wao.
Kikao hicho ambacho hata hivyo kilishindikana kufanyika katika ukumbi na badala yake kufanyika uwanjani kutokana na mafuriko ya umati wa mamia ya wananchi waliojitokeza kumsikiliza Mhe. Mchengerwa ulipambwa na vikundi vya ngoma za asili zilizokonga nyoyo za wananchi waliohudhuria kikao hicho kilichogeuka kuwa zaidi ya mkutano wa hadhara.
Mhe. Mchengerwa alitumia kikaoni hicho kuwaelekeza wananchi jinsi ya kupiga kura na baadaye aliwaombea kura madiwani, yeye mwenyewe katika Ubunge na Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa tiketi ya Urais.

Aidha, Mhe. Mchengerwa alikagua maandalizi ya mkutano ambapo alisema ameridhishwa na maandalizi hayo.
Amewashukuru wananchi wananchi wa Jimbo la Rufiji kwa kuendelea kumchagua katika vipindi vyote kwa kura nyingi na kufafanua kuwa wamekuwa wakimchagua kwa kuwa wamejenga imani kubwa kuwa ni mtumishi wao ambaye siku zote amekuwa na ndoto za kuwaletea maendeleo ya kweli.
Miongoni mwa mafanikio makubwa yaliyoletwa na Mhe. Mchengerwa katika kipindi chake ni pamoja na ongezeko kubwa la Shule za Msingi na Sekondari, zahanati, vituo vya afya na Hospitali, ujenzi wa madaraja, barabara, huduma za maji na kuvutia wawekezaji katika jimbo hilo.