Serikali kupitia Mfuko wa Mawasiliano kwa Wote (UCSAF) inatarajia kuanza utekelezaji wa awamu mpya ya ujenzi wa minara 280 ya mawasiliano, ambapo baadhi ya minara hiyo itajengwa katika maeneo ya mipakani, mbuga za wanyama, na njia kuu za reli za SGR na TAZARA. Hatua hii inalenga kuhakikisha huduma za mawasiliano zinapatikana katika maeneo yote yenye umuhimu wa kimkakati kwa usalama, utalii na maendeleo ya Taifa.
Mtendaji Mkuu wa UCSAF, Mhandisi Peter Mwasalyanda, amesema utekelezaji wa awamu hiyo mpya unafuatia mafanikio makubwa ya mradi wa awali wa minara 758, ambao umefikia zaidi ya asilimia 98 ya utekelezaji.
Ameeleza kuwa kukamilika kwa mradi huo kumechangia kupunguza kwa kiasi kikubwa pengo la mawasiliano katika maeneo ya vijijini na pembezoni. Jumla ya vijiji 1,407 ambavyo awali havikuwa na mawasiliano, sasa vinafikishiwa huduma hiyo muhimu, hatua inayoboresha maisha ya wananchi na kuongeza fursa za kiuchumi.
Aidha, Mhandisi Mwasalyanda ameongeza kuwa utekelezaji wa miradi hiyo unaendana na dhamira ya Serikali ya Awamu ya Sita, inayoongozwa na Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, ya kujenga Tanzania ya Kidijitali na kuhakikisha hakuna mwananchi anayebaki nyuma katika matumizi ya teknolojia ya mawasiliano. Amesema kupitia mradi huo, vijiji vilivyofikishiwa mawasiliano vimeanza kunufaika na huduma za kifedha, elimu, biashara mtandao na fursa nyingine za kidijitali zinazochochea maendeleo ya kijamii na kiuchumi.