Dk Tulia mguu kwa mguu kusaka kura na kuhamasisha ushiriki wa uchaguzi

Mbeya. Mgombea ubunge wa Jimbo la Uyole, Dk Tulia Ackson, ameanza kampeni za nyumba kwa nyumba na mtaa kwa mtaa kuhamasisha wananchi kujitokeza kupiga kura kwa Chama cha Mapinduzi (CCM) katika uchaguzi mkuu utakaofanyika Oktoba 29, 2025, kwa nafasi ya Rais, wabunge na madiwani.

Mbali na hatua hiyo, amekuwa akitembea akiwa na bango lenye picha yake pamoja na mgombea urais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Samia Suluhu Hassan, jambo ambalo limekuwa kivutio kwa wananchi.

Katika kampeni  zake za mguu kwa mguu Dk Tulia leo Oktoba 24,3025 amezifikia kata za Mwasekwa na Ilemi kuhamasisha  wananchi  kujitokeza  kwa wingi kushiriki  uchaguzi  Oktoba29, 2025.

“Jitokezeni kupiga  kura katika uchaguzi  mkuu ili kutimiza haki yenu  kisheria kuchagua Rais, wabunge na madiwani waweze kuleta maendeleo kipindi  cha miaka mitano ijayo,”amesema.

Katika hatua nyingine, Dk Tulia amewataka wananchi kupiga kura kwa amani na kutojihusisha na maandamano au vurugu yoyote, akisisitiza badala yake kulinda amani iliyowekwa na mwasisi wa Taifa, Hayati Mwalimu Nyerere.

“Siku ya Jumatano Oktoba 29, 2025, siku muhimu kwa Watanzania mkapige kura kumchagua  Rais Samia  Suluhu  Hassan  na mimi mbunge  wenu  Dk Tulia, lakini pia madiwani wa kata zote 13 za jimbo la Uyole,” amesema.