BASATA: Sekta ya Sanaa Yakua kwa Asilimia 10, Yachangia Ajira na Uchumi

Dar es Salaam. Afisa Sanaa Mwandamizi kutoka Baraza la Sanaa la Taifa (BASATA), Abel Ndaga, amesema kuwa sekta ya Sanaa ni miongoni mwa sekta zinazokua kwa kasi nchini, ikionyesha ukuaji wa hadi asilimia 10.

Akizungumza jijini Dar es Salaam wakati wa kutangaza kongamano la tatu la Tukutane Dar Arts Week linaloandaliwa na Nafasi Art Space kwa kushirikiana na Serikali ya Norway, Ndaga alisema sekta ya Sanaa imeendelea kuwa nguzo muhimu katika kuchangia uchumi wa taifa na kuinua kipato cha wasanii.

Ndaga alisema Sanaa imeondokana na dhana ya kubezwa, kwani imekuwa ikitoa ajira kwa vijana wengi na kuwa chanzo cha pato kwa serikali kupitia kodi.

“Tunaomba wazazi wawatie moyo watoto wao kushiriki kwenye sanaa kwa sababu ni ajira. Leo ukimuangalia msanii kama Diamond, anaweza kuwaajiri watu zaidi ya 100 hadi 200 kupitia kazi zake. Hii inaonesha wazi kuwa Sanaa ni ajira na pia ni biashara yenye tija,” alisema Ndaga.

Aliongeza kuwa kupitia shughuli za sanaa, wasanii hupata kipato, hulipa kodi na hivyo kuiwezesha Serikali kukusanya mapato zaidi, jambo linalothibitisha kuwa sanaa si uhuni bali sehemu muhimu ya uchumi wa taifa.

Kuhusu kongamano hilo, Ndaga alisema litakuwa jukwaa muhimu kwa wasanii kupata mafunzo, kukuza uwezo, na kujenga mtandao wa kimataifa kupitia ushirikiano na wasanii kutoka nje ya nchi. Hali hii inatarajiwa kuongeza ubunifu, ubadilishanaji wa uzoefu na uzalishaji wa kazi bora zaidi za sanaa.

Kwa upande wake, Mkurugenzi wa Nafasi Arts, Lilian Ipolaiti, alisema Tukutane Dar Arts Week litafanyika kuanzia Novemba 24 hadi 30 mwaka huu, na litajumuisha washiriki takribani 300 wakiwemo wasanii kutoka mataifa mbalimbali yakiwemo Ujerumani, Congo, Uganda na Kenya.