Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe.Balozi Dkt. Emmanuel Nchimbi amesema Taifa limepata pengo kuondokewa na aliyekuwa Mbunge wa Jimbo la Peramiho mkoani Ruvuma, marehemu Jenista Mhagama ambaye alikuwa kiongozi aliyeheshimika na kutumikia nchi katika majukumu mbalimbali ya kitaifa.
Makamu wa Rais amesema hayo wakati akitoa salamu za rambirambi alipowasili kuhani msiba nyumbani kwa aliyekuwa Mbunge wa Jimbo la Peramiho, marehemu Jenista Mhagama eneo la Itega Jijini Dodoma.
Amesema marehemu Mhagama licha ya kuwa ni alikuwa Mbunge wa Jimbo la Peramiho, lakini pia alitoa mchango wake katika Chama Cha Mapinduzi na kusimamia maendeleo ya Mkoa wa Ruvuma kwa ujumla.
Makamu wa Rais ametoa pole kwa familia na waombolezaji na kuwaombea watoto wa marehemu na ndugu wa karibu, Mungu awape ujasiri wa kukubali jambo hilo na kutambua ni njia ya watu wote.






