FYATU MFYATUZI: Tulaani mabeberu mabarubaru na maburebure! Ndivyo ilivyo

Kuna mafyatu wanatubagaza na kutushangaza. Si mabeberu ‘wameleta’ vuguvugu na vurugu kayani!

‘Wamehonga’ watoi na mafyatu wakiwashe na kukinukisha kiasi cha wote kunuka wakahujumu amani ya imani kupitia ‘vurugu’ eti ya kudai haki.

Wamewadanganya kuwashinikiza mdai haki mkaponzwa. Eti hamna haki! Haki gani katika kaya ya amani yenye ajira lukuki? Nani asiyepata haki hadi akataka aipate asiipate kwa vile haipatikani?

Mbona hata wadudu na wanyama kayani wanaipata? Hujasikia chawa, funza, na kunguni wakitesa kama hawana akili nzuri? Hamuoni wanavyozifuja na kuzitabanga njuluku na ‘aslimali’ zetu huku tukisota?

Haki gani mabeberu wanaweza kutoa ambayo hao maburebure hawatoi? Kama yupo asiye nayo, akaitafute ilipo badala ya kuhongwa kutuletea fujo na kutuudhi kwa raha zetu?

‘Wamewahonga’ ndumu, muguka, gongo, na ahadi za unyampala uchwara wauaji na watekaji wasiojulikana kuua na kuteka mafyatu na kuwapoteza mafyatu na mabarubaru wao.

Kwa nini kulaumu mabeberu bila maburebure wakati watekaji hawajulikani, au siku hizi wameanza kujulikana?

Kawaulize akina bashiti walioshiti ukweli na uhalisia wakajifanya hamnazo wasijue kuna siku watalipa si kama walivyotegemea.

‘Wamehonga’ vyombo vya umbea kuandika umbea dhidi maburebure bila kuvisaza vile vya uhasama vinavyotumika kuhalalisha haramu na uovu vya kibeberu ya maburebure kwa maburubaru na mafyatu.

‘Wamehonga’ kila fyatu kuhatarisha maisha ya mabarubaru aka Gen Ziro na mafyatu.

‘Wamehonga’ madoktari ‘kudanganya’ eti walioambwa waue au kuficha namba ya waliouawa! Je, ni wangapi waliuawa na huu ubeberu wa maburebure?

‘Wamehonga’ wazazi kusingiziwa wamefiwa na watoi wakati hawakuuawa! Wamehonga mashehetani waliotishia kukata mafyatu vichwa kiasi cha kushindwa kutumia akili wakiishia kutumia njaa na utumbo. Hawa, ni wabaya kwelikweli.

‘Wamejihonga wakatugeuka bila makosa isipokuwa raslimali zetu. Hata hivyo, hawatutishi.

Nani anahitaji fadhila na misaada yao wakati wanahitaji msaada kuwazuia waache kuhonga na kuharibu mafyatu wetu? Wamejihonga na kujitoa ufahamu na kuanza kutuwekea vikwazo ili tukwazike tujikwaze na wanaotukwaza watukwaze zaidi.

‘Wamehonga’ hata ndege watuzomee na kutushangaa. Kwa nini tunafanyiwa na kufanyiana hivi kana kwamba sisi ni hamnazo au tumejitoa ufahamu na kuwa na kiherehere cha kunyotoana roho?

Mabeberu ‘wanatuonea’ wivu hasa sie wanaotuitao mabureburure wenye mamlaka ya kazi bure kiasi cha kutuzushia mambo ya ajabu. Bure kabisa.

Kufanikiwa, si waliwahonga hata wasioonekana wakawateka, wakawapoteza, na wakawaua mafyatu tena wasio na hatia ili tulaumiwe.

Mwenye makosa anamlaumu asiye nayo. Asiye na makosa anamlaumu kila mmoja kwa kutoshirikiana naye wala kumsaidia kupata jawabu tunalosaka.

‘Wameleta’ bunduki na kuwapa wasiojulikana wauaji wakaua mafyatu halafu wanasingizia ndata wetu watiifu wasioweza kuua hata inzi kama amruisha mkuu wao.

‘Walihonga’ hata vyombo vya umbea vya kimataifa vikadai kuwa mbarubaru waliuawa kwa maelfu wakati waliouawa ni mamluki na si mafyatu wala mabarubaru wa kaya yetu ya peace.

Hata ingekuwa kweli japo ni kweli, nani aliwaua kama siyo mabeberu waliomwaga njuluku? Kwani, yanawahusu nini?

Mambo ya Ngoswe muachia Ngoswe nyie mabeberu hata kama wakati mwingine mnakuwa waungwana na kugharimia sirkal zetu na uchaguzi wetu ili tuwape dili za kuwapiga mafyatu. Hata kama kweli kama tuliua, kwani, tuliua wenu?

Nani kawambia tuliua mabarubaru wetu? Sisi si wanyama kiasi hicho tuue mafyatu wetu. Japo wapo waliokufa, waliuawa na mabeberu siyo sisi walioonyesha ujahiri, ujuha, na uzwazwa vya hali ya juu.

Ebo! Mbona tushaambwa kufa ni kufa na ni jambo la kawaida? Kwani, kwenu ubeberuni, sawa na ububuruni,mabarubaru hawafi kwa mibwimbwi au kujinyotoa roho?

Eti wanataka tufanye mageuzi watugeuze majuha!

Mageuzi kafanye nyinyi. Sisi hatuyahitaji kwa vile ni hatari kwa mstakabali wa kaya yetu ya amani hata kama ni ya imani. Acheni kutuonea wivu.

Tunajua kwanini mnamchukia hata malkia wetu. Mnataka eti tuanzishe domoghasia yenu.

Mbona pale kwa Chaz hawanayo ila mfalme mwenyewe mwana wa maza? Tukiteuana mnasema tuna upendeleo. Mbona Tarampu ameteua wakwe zake na vivyele vyake hamlalamiki? Ni kwa vile sisi siyo watasha siyo?

Wamekuja na kuiba raslimali zetu lakini hawatosheki. Wameingia kimiujiza wakatusainisha mikataba ya uchukuaji ya ajabu ajabu.

Hamtosheki wana hizaya nyie?

Juzi, nilisikia mabeberu na mabuburu wakitaka kupenyeza hata udini! Ebo! Hamjui kuwa hizo dini mlizotuletea zilitukuta na zitatuachana tunajua kuwa mlizitumia kuingiza ukoloni hata uzwazwa kiasi cha kutuibia ardhi, madini, hata majina yetu?

Mnadhani hatujui? Sisi siyo mataahira kama al Shabubu au Buku Haramu kugombania vitu visivyo vyetu wakati tukidharau vyetu.

Sisi ni wazalendo ambao tuko tayari hata kumwaga damu kulinda ulaji, sorry, kaya yetu.

Mkome na kukomaa kabla hatujawakomesha. Senzi nyie. Mnawapa watoi mibwimbwi wachukie wanene wapendwa na wawakosoe wakati hawakosei.

Walaaniwe mabeberu na maburebure. Hivi nshameza vidonge vya kuzuia kuota nchana!