WAZIRI MKUU AKAGUA MRADI UNAOJENGWA KWA USHIRIKIANO NA MRADI WA LNG NA TPDC, LINDI

Waziri Mkuu Dkt. Mwigulu Nchemba leo Desemba 20, 2025 amekagua maendeleo ya mradi wa shule mpya ya msingi ya Likong’o inayojengwa kwa ushirikiano na Mradi wa LNG na TPDC.

Shule hiyo iliyopo katika kijiji cha Likong’o itagharimu kiasi cha shilingi bilioni 1.2 pale itakapokamilika, ambapo kati ya fedha hizo, Serikali imechangia asilimia 26.6, kampuni ya Shell imechangia asilimia 36.6 na kampuni ya Equinor imechangia asilimia 36.6.

Akizungumza na wakazi wa eneo hilo, Dkt. Mwigulu ametoa wito kwa wakazi wa eneo hilo na Tanzania kwa ujumla kuwapeleka watoto wao shuleni kwani Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan ameweka mazingira wezeshe katika sekta ya elimu yanayowafanya watoto wa kitanzania kupata elimu bora.

“Rais Dkt. Samia aliahidi ajira za walimu katika siku 100, sasa usaili umefanyika na walimu 7000 wataajiriwa na itakapofika Januari 10, 2026 walimu hawa wataripoti katika vituo vya kazi watakavyopangiwa”

Naye, Naibu Waziri Ofisi ya Waziri Mkuu-TAMISEMI Reuben Kwagilwa amesema kuwa Rais Dkt. Samia ametoa kiasi cha shilingi bilioni 114 za kushughulikia masuala ya elimu katika mkoa wa Lindi.