PROF.NOMBO:SHERIA YA ELIMU 1978 YAHITAJI MABORESHO MAKUBWA

 

Serikali kupitia Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia na Ofisi ya Waziri Mkuu – TAMISEMI imepokea taarifa ya awali ya Kamati ya Mapitio ya Sheria ya Elimu, Sura ya 353.  

Akizungumza Dodoma, Desemba 30, 2025 katika kikao cha Kisekta cha kupokea taarifa hiyo, Katibu Mkuu wa Wizara hiyo, Prof. Carolyne Nombo, amesema Sheria ya Elimu ya mwaka 1978 imekuwa ikifanyiwa marekebisho mara kwa mara lakini bado ina mapungufu makubwa yanayohitaji maboresho ili kuendana na mageuzi ya kisera na kiutendaji.  

Prof. Nombo alieleza mapungufu hayo ni pamoja na umri wa kuanza shule ya awali na darasa la kwanza, muda wa masomo ya elimu ya lazima na elimu ya awali, kutokuwepo kwa vifungu vinavyotambua wanafunzi wenye mahitaji maalum, ulinzi wa mtoto akiwa shuleni, uimarishaji wa vyombo vya uongozi na usimamizi wa sekta ya elimu pamoja na ushirikiano kati ya sekta binafsi na Serikali katika utoaji wa huduma za elimu.  

Aidha, amebainisha kuwa Kamati iliyoundwa na Wizara Mei 2024 chini ya Prof. Saudin Mwakaje imekusanya maoni ya wadau mbalimbali na kuandaa taarifa ya awali ambayo sasa inawasilishwa kwa uhakiki na maboresho na kisha kwa wadau kama rasimu na hatimae Baraza la Mawaziri.

Mwenyekiti wa Kamati ya Mapitio ya Sheria ya Elimu, Prof. Saudin Mwakaje amesema kuwa Kamati ilifanya uchambuzi wa kina wa matamko ya sera ili kubaini yapi yanahitaji kuwekewa misingi ya kisheria ili kuondoa mgongano kati ya Sera na Sheria. 

Prof. Mwakaje ameongeza kuwa uchambuzi huo ulihusisha wadau mbalimbali wa elimu wakiwemo wakuu wa taasisi za elimu, vyama vya wamiliki wa Shule na Vyuo binafsi, vyama vya kitaaluma, wazazi, walimu, wanafunzi, vyama vinavyoshughulika na Watu wenye welemavu pamoja na wadau wa maendeleo.