Vijana waibua taharuki msibani kisa mwenzao aliyefia mahabusu

Moshi. Ibada ya maziko ya kijana anayedaiwa kujinyonga akiwa mahabusu ya polisi Moshi mkoani Kilimanjaro, Michael Rambau (18) imevurugika baada ya mamia ya vijana ambao ni dereva bodaboda kumvamia kiongozi wa dini aliyekuwa akiongoza ibada hiyo.

Hali hiyo imemfanya kiongozi huyo wa Kanisa Katoliki kuondoka eneo hilo kwa haraka kwa ajili ya usalama wake.


Hata hivyo, vijana hao hawakutaka kusikiliza mahaburi yaliyokuwa yakitolewa na kiongozi huyo wa kiroho wakidai kwa kupiga kelele wakitaka kuambiwa ukweli wa sababu za kifo cha mwenzao.

Mpaka sasa hakuna kinachoendelea katika eneo hilo la mazishi ambapo vijana wa bodaboda wamezingira jeneza lenye mwili wa kijana huyo huku mamia ya waombolezaji wakiwa wamekaa makundi kwa makundi kusubiri hatma ya maziko hayo.


Kijana huyo ambaye ni fundi bomba na dereva bodaboda mkazi wa Mtaa wa Karikacha, Kata ya Rau, mkoani Kilimanjaro anadaiwa kujinyonga kwa kutumia mkanda akiwa mahabusu alikokuwa akishikiliwa Januari 13,2026 kwa tuhuma za kumjeruhi baba mdogo wake kwa kumpiga bapa.

Kwa mujibu wa taarifa iliyotolewa Januari 14, 2016 na Kamanda wa polisi Mkoa wa Kilimanjaro, Simon Maigwa, mtuhumiwa huyo alikuwa akituhumiwa kufanya tukio la mauaji ya baba yake mzazi Novemba 22, 2025 kwa kumchoma na kitu chenye ncha Kali shingoni na kutoroka hadi alipokamatwa Januari 13, kwa kosa la kumshambulia na kumdhuru baba yake mdogo, Brian Felix.

Endelea kufuatilia Mwananchi kwa habari zaidi.