DIRA YA TAIFA YA MAENDELEO 2050 KUWASILISHWA BUNGENI FEBRUARI 2, 2026, UTEKELEZAJI KUANZA JULAI 2026

Na Mwandishi wetu Dodoma .

SERIKALI kupitia Tume ya Taifa ya Mipango imekamilisha maandalizi ya nyenzo kuu tatu zitakazowezesha kuanza kwa utekelezaji wa Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050, ambapo kesho  Februari 2 2026 Dira hiyo inatarajiwa kuwasilishwa Bungeni kwa ajili ya kujadiliwa na hatimaye Bunge kufanya maamuzi.

Akizungumza leo Februari Mosi, mwaka huu jijini Dodoma, Katibu Mtendaji wa Tume ya Taifa ya Mipango, Dkt,Fred Msemwa, amesema Tume hiyo tayari imeanza maandalizi ya utekelezaji wa Dira ya 2050, ambao utaanza kutekelezwa rasmi Julai Mosi, mwaka 2026.

Dkt, Msemwa amesema maandalizi hayo yanalenga kuhakikisha utekelezaji wa Dira hiyo unakuwa wenye mwelekeo, unaopimika na unaoleta matokeo chanya kwa wananchi, sambamba na kuimarisha ushiriki wa wadau mbalimbali wa maendeleo.

Katika hatua nyingine, amesema Tume ya Taifa ya Mipango ipo katika hatua za mwisho za kukamilisha mfumo wa kielektroniki wa ufuatiliaji na tathmini. 

” Mfumo huo utawezesha mageuzi ya ufuatiliaji unaozingatia zaidi matokeo ya kazi, uwajibikaji na ufanisi katika utekelezaji wa mipango ya maendeleo, ” Amesema Dkt, Msemwa.

Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050 ina kauli mbiu ya “Ustawi wa Pamoja”, ikilenga kuhakikisha hakuna Mtanzania yeyote anayeachwa nyuma katika kunufaika na fursa za kijamii, kiuchumi na kimaendeleo zitakazotokana na utekelezaji wa Dira hiyo.

‎Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050 ilizinduliwa rasmi tarehe 17 Julai 2025 na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, ikiwa ni dira inayolenga kulifikisha Taifa katika maendeleo ya juu, ustawi wa watu na mshikamano wa kitaifa ifikapo mwaka 2050.