WAZIRI MKUU, Dkt. Mwigulu Nchemba amesema Serikali imepanga kununua matrekta 10,000 na kuanzisha vituo jumuishi 1,000 vya huduma za zana za kilimo katika ngazi ya Kata, hatua itakayoongeza tija, kupunguza gharama na kuwapa wakulima muda zaidi wa kushiriki shughuli nyingine za kiuchumi.
Ametoa kauli hiyo leo Jumanne, Februari 3, wakati akifungua Mkutano wa Kwanza wa Kikanda wa Afrika wa Matumizi Endelevu ya Zana za Kilimo unaofanyika katika Hotel ya Johari Rotana, Dar es Salaam ambao unalenga kuweka msingi wa ushirikiano wa kikanda katika kuendeleza Ajenda ya Mfumo wa Zana Endelevu za Kilimo Barani Afrika (F-SAMA).
Dkt. Mwigulu amesema ni muhimu kuimarisha uwekezaji katika zana za kilimo rafiki kwa mazingira na zinazozingatia mabadiliko ya tabianchi. “Zana hizi zinapaswa kupunguza uzito wa kazi, kuongeza tija, kupunguza upotevu wa mazao, na wakati huo huo kulinda mazingira kwa kutumia teknolojia zinazohimili athari za tabianchi kama ukame na mabadiliko ya misimu.”
“Tunapaswa kuhakikisha ushiriki mkubwa na wa makusudi wa Sekta Binafsi katika uzalishaji, usambazaji na utoaji wa huduma za zana za kilimo. Serikali zetu zinapaswa kuweka mazingira wezeshi ya sera, sheria na vivutio vya uwekezaji ili Sekta Binafsi iweze kushiriki kikamilifu, kuongeza upatikanaji wa zana za kilimo, na kupunguza gharama kwa wakulima.”
Waziri mkuu amesema kuwa ni lazima kuwawezesha vijana na wanawake kushiriki kikamilifu katika biashara, ubunifu na utoaji wa huduma za zana za kilimo kwa kuwa ni kundi lenye nguvu kazi, ubunifu na uwezo wa kuleta mabadiliko ya haraka endapo litapatiwa mafunzo, mitaji, teknolojia na fursa za masoko.
Amesema uwezeshaji wa makundi hayo ni msingi wa maendeleo jumuishi na endelevu. “Uwezeshaji huu unapaswa kupimwa kwa viashiria mahsusi vya ajira, uanzishwaji wa biashara endelevu, na ushiriki wa vijana na wanawake katika minyororo ya thamani ya zana za kilimo.”
Waziri Mkuu amesema kupitia mkutano huo nchi za Afrika, kwa kushirikiana na Shirika la Chakula na Kilimo la Umoja wa Mataifa (FAO), Umoja wa Afrika (AU), taasisi za fedha, sekta binafsi, watafiti na wadau wa maendeleo zinakusudia kujenga mifumo thabiti ya huduma za zana za kilimo inayokidhi mahitaji halisi ya wakulima wadogo na wa kati, kuimarisha uratibu wa taasisi, kubadilishana uzoefu.
Hivyo, inatarajiwa watunga sera, wataalamu, watafiti, sekta binafsi na washirika wa maendeleo watapata fursa ya kubadilishana uzoefu, kujifunza mbinu bora, na kujenga uelewa wa pamoja kuhusu namna bora ya kuendeleza matumizi endelevu ya zana za kilimo kama chachu ya mageuzi ya mifumo ya uzalishaji chakula.
Kwa upande wake, Waziri wa Kilimo, Godfrey Chongolo amesema kuwa Kupitia mkutano huu, Serikali imepanga kuzindua Mkakati wa Taifa wa Zana za Kilimo wa Awamu ya Pili (2026-2035). Mkakati huu umelenga kuimarisha matumizi, utengenezaji, uendelezaji, uhamasishaji,usimamizi na uratibu endelevu wa teknolojia zinazorahisisha kazi na kuokoa muda katika mnyororo wa uzalishaji na uongezaji wa thamani wa mazao ya kilimo.



