WANANCHI mbalimbali wa Zanzibar wamejitokeza kwa wingi kufungua akaunti katika KCB Bank kwa lengo la kurahisisha na kukuza shughuli zao za kibiashara.
Hatua hiyo imeelezwa kuchangiwa na uzinduzi wa tawi jipya Mkunazini ambapo imeleta urahisi wa shughuli za kifedha kama kutuma miamala pamoja na uhakika wa usalama wa fedha za wateja.
Wakizungumza na waandishi wa habari, akiwemo Leila Seleiman, mkaadhi wa kisiwani hapo na baadhi ya wafanyabiashara walisema kufungua akaunti kutawawezesha kuendesha biashara zao kwa ufanisi na kwa wakati, huku wakiepuka hatari ya kubeba fedha taslimu. Waliongeza pia kuwa huduma za kibenki zitawasaidia kupokea na kutuma malipo kwa urahisi zaidi.
Wananchi wengine wameeleza matumaini yao kuwa hatua hiyo itachochea ukuaji wa biashara binafsi na kuchangia maendeleo ya uchumi wa Zanzibar kwa ujumla.


