Kocha Mtibwa afichua kilichowaangusha | Mwanaspoti

KOCHA Mkuu wa Mtibwa Sugar, Mkenya Yusuf Chippo, ametaja sababu iliyowaangusha wakaambulia kichapo cha mabao 3-1 dhidi ya Mashujaa kuwa ni kutokana na wachezaji kukosa umakini katika eneo la kujilinda.

Katika mechi hiyo iliyopigwa juzi kwenye Uwanja wa Jamhuri jijini Dodoma, mabao ya Mashujaa yalifungwa na Hassan Hadji ‘Cheda’, Jaffary Kibaya na Abdul Bakari, huku la kufutia machozi kwa Mtibwa likifungwa kwa penalti na Fredrick Magata.

Akizungumza baada ya mechi hiyo, Chippo alisema kukosa umakini eneo la kujilinda kulisababisha kufanya makosa yaliyowapa faida wapinzani wao, ingawa kiujumla kiwango cha timu hiyo hadi sasa kinaridhisha na kinampa matumaini makubwa mbeleni.

“Nawapongeza wapinzani wetu kwa sababu walitumia makosa tuliyofanya wakatuadhibu, Ligi ni mbio ndefu na kupoteza kwetu ni somo la kujirekebisha huko mbeleni, tuna wachezaji wazuri sana na wadogo wanaojifunza kila kukicha,” alisema Chippo.

Kichapo hicho cha Mtibwa ni cha kwanza kwa Chippo Ligi Kuu Bara tangu alipojiunga na timu hiyo, Novemba 17, 2025, ambapo kabla ya hapo aliiongoza kwenye mechi nane bila ya kupoteza, huku kati ya hizo akishinda nne tu na kutoka sare pia nne.

Chippo aliyewahi kuzifundisha timu mbalimbali zikiwemo za Pamba Jiji, Coastal Union na TRA United zamani Tabora United, alijiunga na kikosi hicho Novemba 17, 2025, baada ya kuachana na Murang’a SEAL ya kwao Kenya tangu, Agosti 21, 2025.