BASATA YATOA WITO WASANII KUJIRASIMISHA MTANDAONI, TAMASHA LA 17 LA MUZIKI WA CHIGOGO KUFANYIKA JULAI CHAMWINO

…..

Na Carlos Claudio, Chamwino Dodoma.

Baraza la Sanaa la Taifa (BASATA) limetoa wito kwa wasanii wote nchini kujirasimisha rasmi ili waweze kutambulika kisheria na kunufaika na fursa mbalimbali zinazotolewa na serikali, likisisitiza kuwa mfumo wa usajili unapatikana mtandaoni kupitia kiungo cha sanaa.go.tz.

Wito huo umetolewa leo Februari 27, 2026 katika wilaya ya Chamwino, mkoani Dodoma, na Afisa Sanaa kutoka BASATA, Angela Mhilu, wakati wa semina ya viongozi wa makundi yatakayoshiriki Tamasha la 17 la Muziki wa Chigogo litakalofanyika Julai 24–26, 2026 katika viwanja vya Kituo cha Sanaa na Utamaduni Chamwino (CAC).

Angela amesema BASATA imehudhuria semina hiyo kufuatia mwaliko wa CAC kama mdau muhimu wa sanaa nchini, kwa lengo la kutoa elimu kuhusu masuala matatu muhimu ambayo ni urasimishaji wa kazi za sanaa, uandishi wa maandiko ya miradi ya kisanaa, pamoja na mwongozo wa maadili katika utayarishaji wa kazi za sanaa.

“Ni muhimu kwa wasanii kujirasimisha ili kusaidia hata serikali yetu sikivu chini ya Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan kuwa na takwimu sahihi za wasanii,”

“Urasimishaji unarahisisha upatikanaji wa misaada ya kisheria, mikopo kupitia Mfuko wa Utamaduni, elimu ya haki miliki na fursa nyingine mbalimbali,” amesema Angela.

Ameongeza kuwa usajili ni kigezo muhimu kwa msanii kushiriki katika matamasha makubwa yakiwemo yanayoandaliwa na taasisi kama Chamwino Arts Center (CAC)

“Msanii ambaye hajajirasimisha hawezi kushiriki kikamilifu. Ni lazima jamii, nchi na taasisi zinazosimamia sanaa zikufahamu,” amesisitiza.

Kwa upande wake, Mkurugenzi Mtendaji wa CAC, Naamala Samson, amesema mafunzo hayo yameandaliwa kwa viongozi takribani 60 kutoka makundi 50 yanayotarajiwa kushiriki tamasha hilo, kwa lengo la kuwaimarisha katika masuala ya uongozi, fedha na fursa zinazopatikana kupitia COSOTA na Mfuko wa Utamaduni.

“Tumeona ni vyema kuwaandaa mapema ili watimize vigezo vya ushiriki, ikiwemo kujisajili BASATA. Pia tunawapa elimu ya matumizi sahihi ya fedha, uwekaji akiba, uwekezaji na umuhimu wa kujiunga na bima za afya ili kujikinga na majanga,” amesema Naamala.

Amesema tamasha hilo linatarajiwa kuhudhuriwa na zaidi ya watu 5,000, huku mgeni rasmi akitarajiwa kuwa Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Mwigulu Nchemba. 

Aidha, litatoa fursa kwa wasanii kukutana na wadau mbalimbali wakiwemo taasisi, mashirika, makampuni na idara za serikali.

Mratibu wa Tamasha la Muziki wa Chigogo, Sospeter Makana, amesema maandalizi yanaendelea vizuri na makundi zaidi ya 50 yanatarajiwa kushiriki mwaka huu. 

Amesema pamoja na burudani, tamasha hilo litatoa jumbe za maadili na maendeleo kwa jamii.

“Mbali na muziki wa Chigogo, tamasha litakusanya tamaduni kutoka mikoa mbalimbali ya Tanzania. Kutakuwa na vyakula vya asili, mashindano ya upishi, michezo ya jadi kama bao, pamoja na maonesho ya nishati safi ya kupikia kwa bei nafuu kufuatia kampeni ya kitaifa inayohamasishwa na Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan,” amesema Makana.

Ameongeza kuwa Juni 24, 2026 kutafanyika tamasha maalum la watoto litakalowakutanisha wanafunzi na watoto mbalimbali katika viwanja vya CAC kwa ajili ya kujifunza na kuburudika.

Baadhi ya washiriki wa tamasha hilo wameeleza kufurahishwa na maandalizi yanayoendelea. Tadayo Mwingwa, mwalimu wa Kwaya ya Imani tangu mwaka 1995, amesema ameshiriki tamasha hilo kwa miaka 12 na limekuwa na mchango mkubwa katika kukuza umoja na utambulisho wa jamii.

“Nawashauri wasanii ambao hawajawahi kushiriki wachangamkie fursa hii. Tamasha hili linatoa nafasi ya kujifunza na kurithisha utamaduni kwa vizazi vijavyo,” amesema.

Naye mwana historia, Wibberforce Mruka, amesema sanaa na utamaduni ni sehemu muhimu ya taaluma ya historia, akisisitiza umuhimu wa vijana kutembelea vituo vya sanaa ili kujifunza na kudumisha mila na desturi za Kitanzania.

Semina hiyo imelenga kuwajengea uwezo viongozi wa makundi katika maeneo ya uongozi, itifaki, elimu ya fedha, urasimishaji na namna ya kunufaika na fursa mbalimbali kuelekea Tamasha la 17 la Muziki wa Kitamaduni wa Asili ya Chigogo, linalotarajiwa kuwa la kipekee mwaka huu.