UELEWA WA PAMOJA KWA USTAWI WA PAMOJA: WANAHABARI WANOLEWA KUHUSU DIRA 2050

Wanahabari wametakiwa kuwa daraja la kuifikisha kwa umma mikakati na malengo ya Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050 ili kuhakikisha kunakuwepo uelewa wa pamoja utakaowezesha ustawi wa pamoja wa Taifa kwa kipindi cha miaka 25 ijayo.

Wito huo umetolewa na Mgeni Rasmi, Tausi M. Kida, ambaye ni Katibu Mkuu, Ofisi ya Rais–Mipango na Uwekezaji, na Katibu Mtendaji wa Tume ya Taifa ya Mipango, wakati akifungua mafunzo maalumu ya wanahabari kuhusu Dira 2050.

Akizungumza katika mafunzo hayo, Dkt. Kida amesisitiza kuwa mafanikio ya utekelezaji wa Dira 2050 yanategemea kwa kiasi kikubwa namna wananchi wanavyoielewa, kuikubali na kushiriki kikamilifu katika utekelezaji wake.

Amesema wanahabari wana nafasi ya kipekee katika kufafanua sera, mikakati na vipaumbele vya maendeleo kwa lugha rahisi na inayoeleweka kwa umma.

Kaulimbiu ya mafunzo hayo, “Uelewa wa Pamoja kwa Ustawi wa Pamoja,” inasisitiza dhamira ya kuhakikisha kila Mtanzania anafahamu mwelekeo wa Taifa na nafasi yake katika kuifikisha Tanzania tunayoitaka ifikapo mwaka 2050.