MSHAMBULIAJI Said Hamis Said Jr anayekipiga Imigresen, anaendelea kuonyesha makali yake katika Ligi Kuu ya Malaysia baada ya kuwa miongoni mwa wachezaji wanaoibeba timu hiyo.
Said Jr amekuwa na msimu bora na tayari amecheza mechi 21 za ligi akifunga mabao 16 na kutoa asisti nne, takwimu zinazoonyesha mchango wake mkubwa katika kikosi hicho.
Mabao hayo yameisaidia timu hiyo kuendelea kupambania nafasi nzuri katika msimamo wa ligi na kwa sasa ipo nafasi ya nane na pointi 18 baada ya mechi 17.
Huu ni msimu wa kwanza kwa mshambuliaji huyo wa zamani wa Mbao FC kucheza katika ligi hiyo ya Malaysia, lakini ameonekana kuzoea haraka mazingira na kuanza kuonyesha ubora wa kufumania nyavu.
Kabla ya kutua Malaysia, Said Jr aliwahi kucheza katika klabu ya Hatta Club inayoshiriki Ligi Daraja la Kwanza ya Dubai pamoja na Baniyas Club ya Falme za Kiarabu.
Katika safari yake ya soka barani Ulaya, mshambuliaji huyo pia aliwahi kukipiga katika klabu ya FK Jedinstvo UB ya Serbia aliyoitumikia kwa msimu mmoja wa 2023/24.