Wawili mbaroni kupatikana na vipande tisa vya meno ya tembo vyenye uzito wa kilo 30

Mbeya. Jeshi la Polisi Mkoa wa Mbeya linashikilia watu wawili kwa tuhuma za kupatikana na vipande tisa vya meno ya tembo vyenye jumla ya kilo 30, ambavyo vilikuwa vimehifadhiwa kwenye mfuko wa sandarusi.

Kamanda wa Polisi Mkoa wa Mbeya, Benjamin Kuzaga, amesema hayo leo Jumanne, Machi 10, 2026 kwamba watuhumiwa hao wamekamatwa Machi 5 mwaka huu.

Amesema watuhumiwa hao wamekamatwa katika nyumba ya kulala wageni iliyopo Kitongoji cha Jornard, Kata ya Mikoroshini, Tarafa ya Unyakyusa, Wilaya ya Kyela, ambapo meno ya tembo yalipatikana yakiwa yamehifadhiwa kwenye mfuko wa sandarusi.

Kamanda Kuzaga amewataja watuhumiwa hao kuwa Ostin Angetile (40), mkazi wa Ndwanga na Frank Adamson (46), mkazi wa Ngonga, wote wilayani Kyela.

Kamanda wa Polisi Mkoa wa Mbeya, Benjamin Kuzaga akitoa taarifa za misako mbalimbali iliyofanywa mkoani humo. Picha na Hawa Mathias



“Watuhumiwa walikamatwa wakiwa na vipande tisa vya meno ya tembo vyenye uzito wa kilo 30, lakini uchunguzi wa awali umebaini chanzo cha tukio hilo ni tamaa ya kujipatia fedha kwa njia zisizo halali,” amesema.

Kuzaga amesema uchunguzi ukikamilika watuhumiwa watafikishwa mahakamani kwa hatua nyingine za kisheria.

Wakati huo huo, Kuzaga amesema  wanamshikilia Mwinyi Shupika (36) mkazi wa Soweto “B” Kata ya Kasanga, wilayani Chunya kwa tuhuma za kupatikana na bunduki aina ya Shotgan na risasi nane bila kibali.

Kuzaga amesema mtuhumiwa amekamatwa Machi 5, mwaka huu majira ya saa 2.30 usiku na baada Polisi  kupekuwa ndani ya nyumba aliyokuwa akiishi walikuta vitu mbalimbali hususani panga moja, kisu na tochi.

Uchunguzi wa awali umebaini mtuhumiwa anajihusisha na shughuli za uwindaji haramu.

Kuzaga amesema mtuhumiwa anaendelea kuhojiwa na kuomba wananchi wawe mabalozi na kutoa ushirikiano ili kufichua watu wenye viashiria vya uharifu.