Trump Atishia Kuharibu Mafuta ya Iran Ndani ya Dakika Chache

Global Publishers
March 16, 2026
0 Comments

Rais wa Marekani Donald Trump amesema kuwa vikosi vya Marekani vimeshambulia zaidi ya malengo 7,000 nchini Iran tangu kuanza kwa operesheni za kijeshi dhidi ya taifa hilo.

Akizungumza katika hafla moja, Trump alisema pia kuwa zaidi ya meli 100 zimezama katika mashambulizi hayo, akidai kuwa uwezo wa kijeshi wa Iran umeharibiwa vibaya.

“Wameangamizwa kabisa,” alisema Trump, akiongeza kuwa jeshi la anga na jeshi la majini la Iran limepoteza uwezo wake, huku viongozi kadhaa wa kijeshi wa nchi hiyo wakiondolewa madarakani au kuuawa katika mashambulizi hayo.

Trump pia alisema kuwa Marekani kwa kushirikiana na Israel wanafanya kile ambacho, kwa maoni yake, kilipaswa kufanywa miaka mingi iliyopita ili kuzuia vitisho vya kijeshi kutoka Iran.

Kwa mujibu wa Trump, vikosi vya Marekani leo pia vimeshambulia viwanda vitatu nchini Iran vinavyodaiwa kutengeneza ndege zisizo na rubani (drones) na makombora.

Aidha, alikumbusha shambulio la Marekani lililofanywa wiki iliyopita katika Kharg Island, kituo muhimu cha mafuta cha Iran, ambapo alisema karibu miundombinu yote iliharibiwa isipokuwa mabomba ya kusafirisha mafuta.

Hata hivyo, Trump alionya kuwa anaweza kubadili uamuzi wake wakati wowote, akisema kuwa kuharibu kabisa miundombinu ya mafuta ya Iran kunaweza kufanyika ndani ya dakika chache iwapo wataamua kufanya hivyo.

Kauli hiyo inaendelea kuongeza mvutano katika mgogoro unaoendelea kati ya Marekani, Israel na Iran, huku wachambuzi wa siasa za kimataifa wakionya kuhusu hatari ya kuongezeka kwa vita katika eneo la Mashariki ya Kati.