Wanafunzi Wanufaika na Mradi wa Vyoo vya Kisasa Simiyu na Mara

Simiyu & Mara, Tanzania 17Machi 2026: Taasisi ya Vodacom Tanzania Foundation kwa kushirikiana na wadau wake wakiwemo Stanbic Bank Tanzania pamoja na waandaaji wa msafara wa Twende Butiama, wamekabidhi rasmi miundombinu ya vyoo katika Shule za Msingi Sima A iliyopo Bariadi mkoani Simiyu pamoja na Shule ya Msingi Madaraka iliyopo Butiama mkoani Mara.

Mradi huo ni sehemu ya utekelezaji wa ahadi iliyotolewa wakati wa msafara wa waendesha baiskeli wa Twende Butiama uliofanyika Julai mwaka jana, uliolenga kumuenzi Baba wa Taifa Mwl Julius Kambarage Nyerere huku ukihamasisha  maendeleo ya jamii hususan katika sekta za elimu, afya na mazingira.

Kupitia mradi huo, jumla ya matundu ya kisasa ya vyoo 20, kumi kila shule yamejengwa katika shule hizo, hatua inayolenga kuboresha mazingira ya kujifunzia kwa wanafunzi pamoja na kusaidia kulinda afya na ustawi wao shuleni.

Akizungumza wakati wa makabidhiano hayo, Mkuu wa Kanda ya Ziwa wa wa Vodacom Tanzania Plc Ezekiel Nungwi alisema kampuni hiyo inaendelea kushirikiana na jamii katika kuboresha mazingira ya elimu nchini.

“Kupitia taasisi yetu ya Vodacom Tanzania Foundation tunaamini kuwa uwekezaji katika elimu ni uwekezaji katika mustakabali wa taifa. Ujenzi wa miundombinu hii ya vyoo ni sehemu ya kutimiza ahadi tuliyoitoa wakati wa msafara wa Twende Butiama uliofanyika mwaka jana na pia mchango wetu katika kuhakikisha wanafunzi wanapata mazingira salama na bora ya kujifunzia,” alisema Bw Nungwi.

Kwa upande wake, Mwalimu Mkuu Msaidizi wa Shule ya Msingi Sima A Limi Subi aliishukuru Vodacom Tanzania pamoja na wadau wake kwa msaada huo, akieleza kuwa mradi huu utasaidia kuboresha hali ya usafi na afya ya wanafunzi shuleni huku ikiongeza ufaulu wao darasani.

“Ujenzi wa vyoo hivi ni msaada mkubwa kwa shule yetu. Miundombinu hii itasaidia kupunguza changamoto tuliyokuwa nayo ya uhaba wa vyoo na kuwapa wanafunzi mazingira bora na salama ya kujifunzia,” alisema.

Naye Mwalimu Mkuu wa Shule ya Msingi Madaraka Deocray Mtayomba iliyopo wilayani Butiama alisema mradi huo utakuwa na mchango mkubwa katika kuboresha mazingira ya shule na ustawi wa wanafunzi.

“Tunawashukuru sana Vodacom Tanzania Foundation na wadau wao kwa kutukumbuka. Miundombinu hii itasaidia kuboresha usafi wa mazingira ya shule na kuwafanya wanafunzi wawe na muda mwingi zaidi wa kujifunza badala ya kupoteza muda kusubiri huduma ya choo,” alisema.

Mbali na kuboresha miundombinu ya shule, mradi huo pia unalenga kuhamasisha wanafunzi pamoja na jamii kwa ujumla kuzingatia matumizi ya vyoo bora na kuendeleza usafi wa mazingira.

Kupitia miradi yake ya kijamii, Vodacom Tanzania Foundation inaendelea kuwekeza katika maeneo muhimu ya maendeleo ya jamii ikiwemo elimu, afya na mazingira, kwa lengo la kuchangia ustawi wa Watanzania na maendeleo endelevu ya jamii.