China. Waziri wa Viwanda na Biashara, Judith Kapinga ameanza ziara ya kikazi ya siku tatu nchini China yenye lengo la kuhamasisha uwekezaji katika sekta za viwanda na biashara nchini.
Ziara hiyo imeanza katika Jiji la Hangzhou, lililopo katika Jimbo la Zhejiang. Tayari waziri huyo ameshiriki kongamano la wafanyabiashara na wawekezaji takribani 100 lililoandaliwa na China Council for the Promotion of International Trade (CCPIT).
Akizungumza katika kongamano hilo, Kapinga amenadi kwa wawekezaji na wafanyabiashara fursa mbalimbali zilizopo Tanzania katika uwekezaji wa viwanda na biashara, akilenga kuimarisha ushirikiano wa kiuchumi kati ya Tanzania na Jimbo la Zhejiang, hususan katika sekta muhimu za maendeleo.
Waziri wa Viwanda na Biashara, Judith Kapinga akiwa na Mwenyekiti wa CCPIT Jimbo la Zhejiang, Chen Jianzhong.
“Tanzania ina mazingira rafiki ya uwekezaji yanayoweza kuchochea ukuaji wa viwanda na kuongeza thamani ya mazao,” amesema Kapinga.
Amesema kuwa, kwa maana hiyo, Tanzania ni miongoni mwa nchi kitovu cha biashara katika ukanda wa Afrika Mashariki.
Kwa upande wake, Mwenyekiti wa CCPIT Jimbo la Zhejiang, Chen Jianzhong ameahidi kuimarisha ushirikiano wa kibiashara kati ya pande hizo mbili, akibainisha dhamira ya kuhamasisha wawekezaji wa China kuwekeza Tanzania pamoja na kushirikiana katika ujenzi wa viwanda.
Ziara hiyo ya kuvutia uwekezaji wa kimataifa inahusisha makongamano na vikao vya kimkakati vinavyolenga kukuza na kuendeleza uwekezaji nchini.
Baada ya Hangzhou, waziri huyo anatarajiwa kuendelea na ziara katika jiji la Fuzhou lililopo katika Jimbo la Fujian na kuhitimisha katika Jiji la Huizhou, jimboni Guangdong.
