Na Mwandishi Wetu, Pangani
Katibu wa Umoja wa Vijana wa Chama Cha Mapinduzi (UVCCM) wilaya ya Pangani mkoani Tanga, Nasri Mkalipa, ameanza ziara ya kuimarisha uhai wa Chama na kusikiliza kero za wananchi, ziara iliyopewa jina la “Operesheni Samia.”
Mkalipa ameanza ziara hiyo Machi 24, 2026, katika Kata za Mkalamo na Mkwaja ambapo ameonana na makundi mbalimbali ya kijamii ikiwa ni utaratibu wa CCM wa kuwafikia wananchi kule walipo, kusikiliza na kutatua kero zao kwa wakati.
Akiwa ziarani humo, Mkalipa amewaasa vijana kujiunga katika vikundi ili kunufaika na mikopo ya asilimia kumi inayotolewa na Halmashauri. “Vijana wenzangu tujiunge katika vikundi ili tuweze kunufaika na mikopo. Rais wetu na Mwenyekiti wa CCM Taifa, Dk. Samia Suluhu Hassan anatoa fedha nyingi za mikopo, ni jukumu letu vijana kuchangamkia fursa hizo,” amesema Mkalipa.
Sambamba na hilo, Mkalipa amewaeleza vijana kujiandaa kwa ujio wa mashindano ya mpira wa miguu yaliyopewa jina la Aweso Vijana Cup. Katika hatua nyingine, Mkalipa amesema CCM ni Chama imara kinachoaminika na wananchi wake kutokana na sera zake nzuri zinazogusa maisha ya wananchi. Ziara hiyo ya siku tisa itazifikia Kata zote Kumi na Nne za wilaya ya Pangani.

.jpeg)


.jpeg)