Wanawake wajasiriamali kutoka mikoa mbalimbali nchini wamejengewa uwezo kupitia mradi wa Women Creating Wealth (WCW) unaotekelezwa na Shirika la Graca Machel Trust, ukiwa na lengo la kuwawezesha kujikwamua kiuchumi na kukuza mitaji yao ya kibiashara.
Akizungumza leo jijini Dar es Salaam katika mahafali ya wahitimu wa mradi huo, Mratibu wa Women Creating Wealth (WCW), Angaja Mwanga amesema kuwa hadi sasa mradi huo umefanikiwa kuwafikia wanawake wajasiriamali zaidi ya 10,000, hatua inayotarajiwa kuchochea ukuaji wa uchumi wao binafsi pamoja na kuwasaidia kufikia masoko mapana zaidi.
Kwa upande wake, mtoa mada wa mradi huo, Fatma Abdallah Kange amesema wanawake wengi katika jamii wanakabiliwa na changamoto za ukosefu wa ujuzi na uzoefu wa kibiashara, hivyo mafunzo yanayotolewa kupitia mradi huo yanalenga kuziba pengo hilo na kuwawezesha kufanya biashara kwa ufanisi.
Nao baadhi ya wahitimu wa mradi huo, akiwemo Asimin Gombo na Mectlida Godfrey, wameeleza kuwa mafunzo waliyopata yamewajengea uwezo mkubwa wa kuendesha na kukuza biashara zao, pamoja na kuwasaidia kutafuta na kupanua masoko.