Baadhi ya watumishi wa Idara ya Mkaguzi wa Ndani Mkuu wa Serikali, wakifuatilia mada mbalimbali zilizokuwa zikiwasilishwa ikiwemo mifumo ya ukaguzi, rasilimali watu na utawala pamoja na Mfumo wa Usimamizi wa Utendaji Kazi katika Utumishi wa Umma (PEPMIS), katika mkutano wa watumishi wa idara hiyo uliofanyika katika ukumbi wa Olasite, jijini Arusha.
……………
Na. Saidina Msangi, WF, Arusha.
Mkaguzi wa Ndani Mkuu wa Serikali, Bw. Benjamin Magai, amewapongeza Watumishi wa Idara hiyo kwa kuendelea kufanya kazi kwa bidii na uadilifu hivyo kuiwezesha Idara kufikia malengo yaliyopangwa.
Bw. Magai alitoa pongezi hizo wakati akifunga Mkutano wa Watumishi wa Idara ya Mkaguzi wa Ndani Mkuu wa Serikali, uliofanyika katika ukumbi wa Olasite Garden, jijini Arusha.
Alisema Watumishi wa Idara hiyo wameonesha weledi na uadilifu katika kutekeleza majukumu yao ikiwemo ufuatiliaji wa ripoti mbalimbali za kiutendaji kama ilivyotarajiwa.
‘‘Kwa kweli niwapongeze kwa utendaji kazi mzuri na nikiri sijapata kesi zozote za maadili hivyo tuendelee kutunza maadili kwani mkaguzi hutakiwi kuwa na tuhuma zozote maana inashusha hadhi ya Idara ikumbukwe kuwa tunaowakagua wanajifunza kwetu’’, alisisitiza Bw. Magai.
Aliongeza kuwa kikao hicho kimekuwa na tija kwani kimetoa fursa kwa watumishi kujadili mafanikio na changamoto mbalimbali pamoja na kuweka mikakati ya kuboresha utendaji kazi.
Aidha, Bw. Magai aliwasisitiza watumishi hao kuwa licha ya kuendelea kutekeleza majukumu yao kwa weledi ni vema pia kujiandaa na maisha ya baadaye baada ya kustaafu ili kuwa na maisha bora.
Mkutano huo wa siku mbili uliwakutanisha Watumishi wa Idara ya Mkaguzi wa Ndani Mkuu wa Serikali kwa lengo la kujadili mafanikio, changamoto, na njia bora za kuboresha utendaji kazi kwa manufaa ya umma kwa kuhakikisha uwajibikaji na matumizi bora ya rasilimali za umma.