Mwandishi wa NCAA, Arusha.
Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Philip Isdor Mpango amesema eneo la Hifadhi ya Ngorongoro ambalo ni urithi wa dunia linapaswa kuendelea kutunzwa kama fahari ya nchi ili liendelee kuwa kimbilio la wageni wengi wanaokuja Tanzania kwa shughuli za utalii.
Dkt. Mpango ameeleza hayo wakati alipotembelea banda la Mamlaka ya Hifadhi ya Ngorongoro wakati wa ufunguzi wa mkutano wa Pili wa mabaraza huru ya Habari Afrika (The 2nd Pan-African Media Council Summit) katika ukumbi wa mikutano wa AICC Jijini Arusha leo tarehe 15 Julai, 2025.
“Eneo la hifadhi ya Ngorongoro sio tu ni urithi wa Tanzania bali kwa dunia nzima, endeleeni kulitunza na hakikisheni mnahamasisha wananchi wengi hasa wa nje ya Mkoa wa Arusha kuja Ngorongoro kuona fahari ya Nchi yetu” amesema Dkt. Mpango.
Akitoa maelezo kwa Mhe. Makamu wa Rais, Afisa Utalii Mkuu kutoka NCAA PCOI Peter Makutian ameeleza kuwa pamoja na kuimarisha shughuli za uhifadhi, eneo la hifadhi ya Ngorongoro lina vivutio vingi na vya kipekee kama kreta za Ngorongoro, Empakai, Olmoti, Mlima Lolmalasin ambao ni wa tatu kwa urefu Tanzania, Makumbusho ya Olduvai Gorge, Mchanga unaohama, Nyayo za Laetoli, tambarare za Ndutu ambapo ni mazalia ya Nyumbu wanaohama, maporomoko ya maji endoro pamoja na kusimamia vituo vya mambokale ambayo ni Mapango ya Amboni Tanga, Kimondo cha Mbozi, Magofu ya Engaruka na Mapango ya Mumba.
Maktutian pia amemueleza mhe. Makamu wa Rais kuwa hivi Karibuni eneo la hifadhi ya Ngorongoro lilipata tuzo ya kuwa Kivutio bora cha Utalii Afrika kwA mwaka 2025 ikiwa ni mara ya pili baada ya kushinda tuzo hiyo mwaka 2023.
Mkutano wa pili wa mabaraza huru ya Habari Afrika ulioanza jana tarehe 14 unaendelea hadi tarehe 17 julai 2025 na unakutanisha zaidi ya washiriki 200 kutoka mataifa mbalimbali ya ndani na nje ya Bara la Afrika ambapo NCAA inatumia mkutano huo kunadi vivutio vya utalii kwa washiriki wa mkutano huo.