Madereva 42 wakiwepo wa masafa marefu wamefungiwa leseni

Mbeya. Jeshi la Polisi kupitia Kitengo cha Usalama Barabarani mkoani Mbeya limezifungia leseni 42 za madereva, wakiwemo madereva wa masafa marefu, baada ya kubainika kukiuka sheria na kanuni za usalama barabarani kwa kuendesha kwa mwendo hatarishi.

Hatua hiyo imechukuliwa kama sehemu ya mkakati wa kupambana na ajali za mara kwa mara, kwa kutumia mfumo wa Ufuatiliaji wa Mwenendo wa Magari (Vehicle Tracking System – VTS), katika maeneo mbalimbali ya Mkoa wa Mbeya.

Akizungumza leo Ijumaa, Julai 18, 2025, wakati wa mpango maalumu la ukaguzi wa mabasi ya abiria katika Kituo Kikuu cha Mabasi ya Mikoani, Mkuu wa Kikosi cha Usalama Barabarani Mkoa wa Mbeya (RTO), Mrakibu Mwandamizi wa Polisi, Notka Kilewa, amesema kuwa leseni hizo zimefungiwa kwa kipindi cha miezi mitatu, huku uchunguzi na ufuatiliaji ukiendelea ili kudhibiti ukiukwaji wa sheria za barabarani.

Ukaguzi huo uliongozwa na Mkuu wa Kikosi cha Usalama Barabarani nchini, Naibu Kamishna wa Polisi, Fraisser Kashai kutoka Kamisheni ya Mafunzo, ukiwa na lengo la kuhakikisha magari ya abiria yanazingatia vigezo vyote vya usalama kabla ya kuanza safari.

SSP Kilewa aliongeza kuwa katika kipindi cha Januari hadi Juni mwaka huu, jumla ya madereva 42 wamefungiwa leseni kutokana na makosa mbalimbali ya kihatarishi.

Miongoni mwa makosa hayo ni pamoja na kuendesha kwa mwendo kasi, kuyapita magari mengine katika maeneo yasiyoruhusiwa, pamoja na ulevi wakati wa kuendesha magari.

Mkuu wa Kikosi cha Usalama Barabarani Mkoa wa Mbeya (RTO),  Mrakibu Mwandamizi wa Polisi, Notka Kilewa amesema leo Ijumaa Julai 18,2025 wakati wa zoezi la ukaguzi  maalumu wa  mabasi ya abiria kabla ya kuanza safari.

Ukaguzi huo umefanyika katika kituo kikuu cha mabasi ya mikoani na kuongozwa na Mkuu wa Kikosi cha Usalama Barabarani nchini  na Naibu Kamishna wa Polisi, Fraisser Kashai kutoka Kamisheni ya Mafunzo.

Kilewa amesema wataendelea  kuwachukulia hatua za kisheria  madereva wanaokiuka sheria sambamba na  kuwafungia leseni kwa kipindi cha  miezi mitatu, lakini kwa  kipindi cha Januari hadi Juni, mwaka huu madereva 42 wamefungiwa leseni.

Ametaja baadhi ya makosa hatarishi yaliyopelekea kufungiwa leseni ni pamoja na mwendo kasi, kuyapita magari mengine katika maeneo yasiyoruhusiwa, ulevi wa pombe wawapo safarini.

“Tutaendelea kukabiliana  nao  na kuwachukulia hatua, lakini tuwatake kutoa madereva kutoa  taarifa za wamiliki wenye  mabasi mabovu au dosari ili waweze kufuatiliwa na kuwachukulia hatua kwa kutambua  wao ndio  wanaopata shida na wawapo barabarani,” amesema.

Katika hatua nyingine, Kilewa  ameonya madereva kuhepuka tabia za ulevi kukimbizana wawapo safarini ili kudhibiti ajali za barabarani  zisizo za lazima na kulinda maisha ya abiria na mali zao.

Awali akizungumza baada ya kufanya ukaguzi  wa mabasi DCP Kashai ametoa tahadhari kwa madereva kuheshimu na kutii sheria ili kuhepuka ajali zisizo za lazima.

Pia, ameisisitiza madereva kutii sheria   kwani watakao kiuka na kubainika  watachukuliwa hatua za kisheria sambamba na kufungiwa leseni.

Miongozi wa ukaguzi uliofanywa ni pamoja na  mabasi ya  abiria, leseni za madereva,  kupima kilevi sambamba  na utoaji elimu ya usalama barabarani kwa abiria  lengo kufanya ufuatiliaji na  utekelezaji wa maagizo ya Serikali.

Ofisa Mfawidhi wa  Mamlaka ya Udhibiti  Usafiri wa Ardhini (Latra)  Mkoa wa Mbeya, Shaban Mdende amesema  katika kukabiliana  na ajali za barabarani mabasi ya abiria yamefungwa kifaa maalum cha kudhibiti mwendo.

“Latra tunashirikiana na Polisi usalama barabarani  kufanya ufuatiliaji wa mwenendo  wa mabasi kwa kutumia kifaa maalumu cha VTS , ambapo kwa kipindi cha Januari hadi Juni  kati ya madereva 42 waliofungiwa leseni  26 ni walibainika  kupitia mfumo huo,” amesema.

Mkazi wa eneo la Kabwe jijini hapa, Johnson Elius amesema licha ya jitihada za Jeshi la Polisi na Latra kukabiliana  na uzembe wa madereva kukiuka sheria bado,  kuna maeneo wamekuwa wakishindana kwa kuendesha mwendo kasi.

“Tuishauri Serikali katika kukabiliana na ajali nyingi za barabarani iongeze nguvu ya kufunga mifumo ya kamera  maeneo hatarishi  ambayo hayana askari wa usalama barabarani  jambo ambalo litaleta tija kubwa na kukomesha madereva  wazembe,” amesema.