Hosptali ya Kanda Mbeya kuboresha huduma ya uangalizi watoto

Mbeya. Katika kuhakikisha huduma bora za uangalizi wa watoto walizaliwa kabla ya muda, Hosptali ya Rufaa Kanda ya Mbeya imenufaika na vifaa tiba vya kisasa (Monitor) 15 kutoka kwa Wadau wa Maendeleo Tanzania.

Vifaa hivyo vimekabidhiwa leo Jumamosi  Agosti 16, 2025 na Meneja wa  Kampuni ya Goal 3 Tanzania, Mwamvua Mika  kwa Kaimu Mkurugenzi  Mtendaji  wa Hospitali  ya Kanda ya Mbeya,Dk Myriam Msalale.

Amesema vifaa tiba hivyo tayari vimefungwa na kuanza kutoa huduma lengo ni kuhakikisha watoto wachanga wanaozaliwa kabla ya muda  wanapata huduma bora kama sehemu ya kuunga mkono Serikali ya awamu ya sita katika kugusa sekta ya afya.

“Tumefunga vifaa tiba vya kisasa  kwenye kitengo cha Niku ili kuboresha huduma kwa watoto wachanga ,lakini pia tushukuru uongozi  wa Hosptali kwa ushirikiano  mzuri wa hatua kwa hatua hadi kufanikisha kufunga  monitor 15 ambazo  kimsingi  zitaleta chachu kubwa katika kuboresha utoaji wa  huduma bora, “amesema.

Awali,  akizungumza baada ya makabidhiano ya vifaa hivyo, Kaimu Mkurugenzi  Mtendaji  Hosptali  ya Rufaa  Kanda ya Mbeya,  Myriam Msalale amewashukuru wadau  kwa kuguswa  kuchagia vifaa tiba vya kisasa  ambavyo vitahochea uboreshwaji  wa huduma kwa watoto wachanga  walio kwenye uangalizi .

Amesema kimsingi  vimekuja wakati mzuri na kwamba vitaleta tija katika kuboresha huduma kwa watoto wachanga wanaozaliwa kabla ya muda, lakini  pia nisisitize  vitumike kwa uangalizi mkubwa.

“Nitake tu vitaatiba hivyo kwa kisasa ambavyo leo tumekabidhiwa na wadau wa maendeleo  visimamiwe vyema ili viweze kudumu kwa muda mrefu katika kuboresha huduma ya watoto wanao zaliwa kabla ya muda na kufikishwa kwenye kitengo hicho,”amesema.

Daktari Bingwa mbobezi wa watoto wachanga, Dk Rehema Marando amesema vifaa tiba hivyo  vitaleta tija kubwa ya kuboresha ufanisi wa utoaji wa huduma za matibabu na uangalizi  kwa watoto.

“Kimsingi  sasa huduma zitaboreshwa zaidi lakini tunashukuru  wadau wa maendeleo  kwa hatua hiyo nzuri ya kugusa na kuongeza ufanisi wa  vifaa  tiba kwa ajili ya watoto wachanga kikubwa tunashukuru, “amesema.

Mkazi wa Soko la Matola jijini hapa,  Rehema Mwanjonde amesema hatua ya wadau kugusa huduma  za afya kwa watoto wachanga ni ishara kubwa ya ushirikiano na  serikali iliyopo madarakani na kuomba wengine kuguswa kuchangia ili kunusuru  vifo visivyo vya lazima.